WIZARA YA AFYA YAIKABIDHI ZIMAMOTO MAGARI YA UOKOAJI YENYE THAMANI YA BILIONI 1.6

Na. Catherine Sungura,Dar es salaam.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu leo Julai 8, 2023 amemkabidhi Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Inj. Hamad Masauni Magari matatu ya uokoaji yenye zana za kisasa yenye thamani ya shilingi Bilioni 1.6 kwa ajili ya jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwenye hafla fupi iliyofanyika viwanja vya Zimamoto mkoa wa Ilala jijini Dar es salaam.

Waziri Ummy amesema magari hayo yamekuja wakati muafaka ambapo kwa sasa dunia inajiandaa kukabiliana na majanga, dharura na magonjwa ya milipuko hivyo magari hayo yataenda kutoa huduma za awali pindi ajali inapotokea ili kupunguza madhara yatokanayo na ajali au vifo.

Amesema Wizara yake ilianzisha mfumo rasmi wa huduma za dharura nje ya hospitali ikiwemo uokoaji wakati wa ajali ili kuwezesha majeruhi wa ajali kupata huduma ya kwanza eneo la tukio kabla ya kusafirishwa kwenye vituo vya kutolea huduma za tiba.

“Huwa naumia sana ajali inapotokea unaona mtu mzima au mtoto anateketea kwa kukosa vifaa vya uokoaji , kwahiyo mfumo huu wa huduma za dharura nje ya hospitali (EMS) ni hatua muhimu utakaoweza kupunguza athari kwa majeruhi ikiwemo ulemavu pia gharama za matibabu kwa Serikali, mwananchi pamoja na vifo”.

“Magari haya yana uwezo wa kunyanyua na kukata vyuma (Rescue Vans) ambayo pamoja na kazi nyingine yataweza kuopoa majeruhi walionasa katika magari yatakayopata ajali na kazi hii itafanywa vyema na wenzetu wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji”. Amesema Waziri Ummy

Hata hivyo Waziri Ummy amesema mradi huo umekuja kipindi ambacho kumekuwepo na ongezeko la ajali za barabarani nchini na duniani kote hususan nchi zinazoendelea, “Takwimu zinaonyesha kwamba duniani kote inakadiriwa kuwa hutokea ajali za barabarani zipatazo milioni 1.3 kila mwaka.

Kwa upande wa takwimu kwa hapa nchini Waziri Ummy amesema kumekuwa na ongezeko kubwa la majeruhi wa barabarani ambapo 47% ni majeruhi watokanao na ajali za pikipiki na jumla ya majeruhi wa ajali walioingia kwa dharura katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na Taasisi ya Tiba ya Mifupa (MOI) kwa mwaka 2021 walipokea majeruhi wa ajali 9,270 na mwaka 2022 walipokea majeruhi wa ajali barabarani 9,933.

“Waziri tutaleta taarifa ili kuweka mikakati ya kudhibiti ajali za barabarani ikiwemo ajali za pikipiki kwa kuangalia ubora wa ‘helmet’ zinazoingizwa hapa nchini kwani tumeona haziwasaidia watu wengi na kwa bahati mbaya upasuaji wa majeruhi wa ajali watu wengi hawawezi kumudu gharama za matibabu na wengine hawana bima ya afya, na hivi sasa nina vijana wengi ambao ndio nguvu ya Taifa wanahitaji miguu bandia”.

Pamoja na hayo Waziri Ummy amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mara ya kwanza katika uongozi wake kuweza kujenga majengo ya dharura (EMD) hadi ngazi za wilaya yapatayo majengo 81 na hospitali za mikoa majengo 21 pia wodi za wagonjwa mahututi (ICU) 28 katika hospitali za wilaya na 45 katika hospitali za Mikoa, Kanda na Taifa.

Naye, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Inj. Hamad Masauni ameishukuru Wizara ya Afya kwa kuwapatia magari hayo ambayo yanaenda kuongeza tija na kuondoa changamoto zilizokuwa zinaikabili jeshi hilo na kuahidi kuyatumia magari hayo ipasavyo.

Amesema magari hayo ni dhamira na mapinduzi makubwa katika jeshi hilo inayofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona jeshi hilo linakua na vifaa na zana za kisasa katika uokoaji.

“Ni kweli ajali za barabarini zinaangamiza maisha ya watu wengi hivyo kwa mradi huo utaenda kuwasaidia wananchi kwani tayari askari wameshapatiwa mafunzo na kuwa na weledi katika utoaji wa huduma za uokoaji.

By Jamhuri