Kikosi cha Yanga kesho kitashuka dimbani Uwanja wa Namfua kwa ajili ya kucheza dhidi ya Singida United kutafuta nafasi ya kutinga hatua ya nusu fainali Kombe la FA.

Yanga ambayo ilikuwa imeweka kambi ya muda mfupi mjini Morogoro, tayari ipo Singida huku ikielezwa wachezaji wake wote wapo fiti kiafya.

Kwa mujibu wa Afisa Habari wa Yanga, Dismas Ten, amesema wachezaji wote wapo sawa kuelekea mchezo huo, na jukumu limesalia kwa Mwalimu, George Lwandamina, kuamua nani amuanzishe.

Singida itakuwa inaikaribisha Yanga ikiwa na kumbukumbu za kulazimishwa sare ya bao 1-1 kwenye mechi ya ligi ya mzunguko wa kwanza iliyopigwa Namfua Stadium.
Timu itakayoshinda katika mechi hiyo itaungana na Stand United ya Shinyanga kwenye hatua ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho iliyotinga jana kufuatia ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Njombe Mji FC.

By Jamhuri