Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia,Kibaha

Baadhi ya wakazi wa eneo la Shirika la Elimu Kibaha ,Tumbi wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji takriban miezi mitano, hali ambayo inasababisha kununua dumu la maji kwa sh.500 kwa kusafirisha na pikipiki.

Kutokana na kero hiyo,wameiomba Mamlaka ya Usafi wa Mazingira na Majitaka (DAWASA) Kibaha kuwasaidia kutatua hali hiyo kwani wanapata shida.

Cresencia Shirima Balozi wa Kanda, alieleza ,wamekosa huduma ya maji tangu mwezi wa nne hali ambayo inasababisha kupata kero katika matumizi ya maji .

Shirima alieleza, wamekuwa wakinunua maji sehemu nyingine ambapo wananunua dumu la lita 20 kwa shilingi 500 na gharama ya kuyasafirisha ambapo hutumia pikipiki.

“Watu wanafamilia na zina watoto wadogo ambapo huwalazimu watafute kwanza maji ndipo waende kazi hali ambayo inasababisha kuchelewa kazini kwani hawawezi kuondoka bila ya kuacha maji nyumbani,”alisema Shirima.

Alifafanua wapo, mjini hawapaswi kuteseka kama vile wako Kijijini na zinaweza kutokea athari za kiafya.

Kwa upande wake Optatus Katata alisema , waliongea na viongozi wao lakini hakuna maji na wanaomba Dawasa iwatatulie kero hiyo kwani wamekuwa wakiahidiwa muda mrefu ambapo maeneo jirani hakuna tatizo hilo.

Naye Imani Kayombo alieleza, maji waliambiwa kuwa msukumo wa maji ni mdogo hivyo maji kushindwa kufika kwenye maeneo yao hivyo huwabidi kufuata maji mbali.

Kayombo alisema kutokana na changamoto hiyo hutumia gharama kubwa kwa kutumia shilingi 10,000 kwa ajili ya kupata maji lakini wanasema kama wangepata huduma hiyo wasingepata gharama kubwa kiasi hicho.

Mabuba Toksini kuwa imefikia hatua wanachukua maji sehemu wanazofanyia kazi ambapo maji ni uhai na siyo anasa na wananunua maji kutoka kwa magari yanayouza maji mtaani.

Toksini alisema kuwa tatizo ni kubwa sana na Dawasa hawatoi taarifa juu ya tatizo lililoko ma kama ingewezekana wangewapatia maji angalau mara moja kwa wiki na anashangaa kuletewa ankara ambapo maji hayatoki na hata yakitoka ni usiku wa manane na yanatoka sehemu za bondeni na kwa muda mfupi.

Kwa upande wake meneja wa Dawasa Kibaha Alfa Ambokile alisema kuwa changamoto hiyo inafanyiwa kazi kwa kuwa eneo hilo lina mradi na unaendelea kufanyika.

Ambokile alisema kuwa mradi huo utakapokamilika utaondoa changamoto hiyo kwa wakazi hao wa Tumbi na Mwanalugali na hali itarejea kama kawaida.

By Jamhuri