Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Alhaji Jabir Shakimweri ameipongeza Benki ya Akiba kwa juhudi na jitihada zake katika kuboresha na kuhifadhi mazingira na kusistiza taasisi nyingine kuiga mfano huo .

Pongezi hizo amezitoa leo Dodoma katika hafla ya uzinduzi wa viunga vilivyobereshwa vya independence Square na kukabidhi rasmi awamu ya pili ya uboreshaji viwanja hivyo ambapo benki imekuwa ikijitolea shughuli za kijamii ikiwemo kuhifadhi na kutunza mazingira, samba samba na kaulimbiu ya Siku ya Mazingira Duniani ya mwaka huu, isemayo “Our Land, Our Future” – “Ardhi Yetu, Mustakabali Wetu,” ambayo imebebwa na mada kuu ya “Land restoration, desertification and drought resilience” ambayo inalenga urejeshaji (utunzaji) wa ardhi, kupambana na uzalishaji wa majangwa, na ukame.

“Leo ni siku ya Maadhimisho ya Mazingira Duniani Benki ya Akiba katika kusaidia mapambano dhidi ya ukame na majangwa watu wote kila mmoja ana jukumu la kulinda na kuhifadhi mazingira ili kuhakikisha dunia inabaki kuwa mahali salama pa kuishu kwa sasa na vizazi vijavyo” amesema Mkuu wa Wilaya

Naye Meneja wa tawi la Dodoma la Benki ya Akiba, Bi. Upendo Makula, amesema Benki ya Akiba imekuwa ikishiriki kikamilifu katika uhifadhi wa mazingira kwa namna mbali mbali kuanzia kupitia huduma zake na ushiriki wa katika shughuli mbali mbali za kijamii pia imepunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya karatasi kwa kuboresha huduma zake za kidijitali, zikiwemo Akiba Mobile, Akiba Wakala, kadi za VISA, taarifa za kielektroniki (E-statement), na huduma za benki Mtandao (Internet Banking).

Sanjari na hayo amebainisha kuwa huduma hizo si tu kwamba zinapunguza matumizi ya karatasi, bali pia huleta urahisi na uhakika, na kukidhi mahitaji ya soko kwa ufanisi hata hivyo benki hiyo inatoa huduma mbalimbali kama mikopo, akaunti, na bima, zinazowafikia wateja tofauti kuanzia mtu binafsi hadi makampuni makubwa na taasisi za serikali.

Aidha Bi. Makula alibainisha kuwa Akiba Commercial Bank inashiriki kikamilifu katika shughuli za jamii za kuhifadhi mazingira kama sehemu ya Sera yake ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR). Mfano halisi ni jitihada zake za muda mrefu za kutunza na kuboresha viwanja vya Independence Square huko Dodoma, jukumu ambalo limekuwa likitekelezwa kwa zaidi ya miaka kumi. Juhudi hizi zinaonyesha nia thabiti ya benki hiyo ya kutunza na kuhifadhi mazingira kwa ajili ya urithi bora wa vizazi vijavyo.