Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere amebaini kuwepo kwa mapungufu ya utandaji umeme vijijini na kuashiria kuwepo kwa mianya ya ubadhirifu wa fedha.

Hayo yamebainika katika ripoti yake ambapo katika ukaguzi Mamlaka ya Nishati Vijijini (REA),ambapo CAG amebaini kuwa transfoma zilizofungwa uwezo wake ni 50KV, wakati bajeti ilikuwa 100KV.

CAG ameimulika REA kuanzia mwaka 2015/2016 mpaka 2019/2020.

Ukaguzi umefanyika kwa maombi ya wafadhili; Shirika la Kimataifa la Maendeleo Sweden (Sida).

Kwamba Machi 2016, Tanzania na Sida waliingia mkataba wa ufadhili wa kutandaza umeme vijijini. Fedha zilitoka SEK 600 milioni (Sh133 bilioni).

Uzembe wa kuchelewa kupakua malighafi Bandari ya Dar, ulisababisha REA watumie Sh775.76 milioni kulipa tozo ya uchelewaji (demurrage charge). Fedha za ufadhili zikatumika ndivyo sivyo kwa uzembe.

Ripoti hiyo ilibaini kuwa upembuzi yakinifu haukufanyika. Hata udongo haukupimwa. Nguzo zimewekwa pasipo vipimo. Pesa ya upembuzi yakinifu (feasibility study), haijulikani ilipo.

Wateja 51,425 tu kati ya 98,689 walioomba kuunganishiwa umeme, ndio wameungabishiwa. Hiyo ni sawa na asilimia 52.1.

CAG ameandika; nyaraka za Sida zinaonesha REA walitakiwa kusambaza umeme kwenye nyumba 86,000, hivyo kuhudumia watu 430,000 kupitia gridi ndogo (Green Min and Micro Grid). Wameishia nyumba 17,302, yaani asilimia 20.

Uzembe wa kutohuisha taarifa za utafiti wa mradi, ulisababisha REA kuingia gharama za ziada Sh160 milioni.

Kuna jumla ya Sh5.94 bilioni, ambazo REA wamekuwa wakizitenga kama bajeti ya matangazo na elimu lakini hakuna maelezo ya zilivyotumika.

Mwaka 2018/2019, REA walitengeneza bajeti ya kununua transfoma na kuunganishia wateja umeme Sh254.8 bilioni. CAG akagundua, gharama halisi ilikuwa Sh117 bilioni. Kwa hiyo kulikuwa na udanganyifu wa Sh137.8 bilioni. Ufisadi.

Lingine, REA wilitumia Sh125.57 milioni, kununua transfoma 12 zilizo chini ya kiwango.

Siasa zikaingia. Tozo ya umeme kwa mwezi ikapitishwa Sh11,000. Serikali ikasema tozo Sh1,000. Gharama za uendeshaji zikawa kubwa kuliko mapato. Umeme ukazima vijijini.

Sehemu kubwa, CAG ameeleza tatizo la uchelewaji. Miradi ambayo ilipaswa kukamilika mwaka 2019/2020, mpaka sasa bado.

Hayo yalitokea Waziri wa Nishati akiwa Kalemani, aliyempokea Simbachawene kutoka kwa Muhongo, Rais akiwa Magufuli.

By Jamhuri