Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Mkuranga

SERIKALI ya Canada kupitia ‘CARE International Canada’ imetenga takribani CAD 20 milioni (Shilingi Bilioni 38) zitakazo tekeleza Mradi wa “Her Resilience, Our Planet Project”.

Miradi huo unalenga kuongeza ushiriki wa vijana na wanawake katika shughuli za kiuchumi sambamba na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kupitia teknolojia za kibunifu na kanuni za kilimo endelevu.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi huo hivi karibuni katika Shamba la Miembe wilayani Mkuranga mkoani Pwani, Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa wa Canada, Ahmed Hussen, alisema mradi huo utatekelezwa ndani ya miaka sita na hivyo kuchochea kilimo endelevu na kuongeza fursa za ajira kwa vijana na wanawake nchini.

“Kupitia mradi huu, Serikali ya Canada kwa kushirikiana na Tanzania tutahimiza uwajibikaji katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuzingatia maeneo matatu muhimu: kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kupunguza madhara yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi, sambamba na mpito wa nishati mbadala,” amesema Waziri Hussen.

Waziri Hussen ameeleza umuhimu wa maendeleo endelevu na shirikishi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kusisitiza dhamira ya Kanada ya kufikia malengo ya maendeleo endelevu kwa ushirikiano na Tanzania.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde mbali ya kuishukuru Serikali ya Canada kupitia ‘CARE International Canada’ kwa ushirikiano wao katika kutatua changamoto zinazowakabiliza kimataifa alihakikisha uungaji mkono wa mradi huo.

“Ziara yenu inadhihirisha ushirikiano imara uliopo kati ya mataifa yetu katika kukabiliana na changamoto kubwa za kimataifa, ikiwemo mabadiliko ya tabianchi na maendeleo endelevu,” amesema Waziri Silinde.

Amesema kilimo kinaajiri zaidi ya asilimia 80 ya watu wote ni uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania, lakini mabadiliko ya tabianchi yamekwamisha kwa kiasi kikubwa uzalishaji na hivyo kuwaingiza wengi katika umaskini na uhaba wa chakula.

Waziri Silinde amesema lengo la mradi huo ni kuongeza uwezo wa wakulima zaidi ya 175,000, kwa vijana na wanawake, ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kupitia teknolojia ya kibunifu na kanuni za kilimo endelevu.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakary Kunenge, ameshukuru ziara ya Waziri Hussen na kusisitiza ari ya serikali katika kuinua na kuboresha kilimo ikiwa ni pamoja na kuanzisha miradi ya kimkakati kama BBT. Alimhakikishia Waziri dhamira ya serikali ya mkoa katika kusimamia na kutekeleza vipaumbele vya Serikali.

Naye mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa SAGCOT, Tula Mloge, mbali ya kupongeza ushirikiano wa Canada na Tanzania katika kuchochea na kukuza kilimo nchini alisisitiza dhamira ya kituo hiko ya kukuza kilimo endelevu na chenye tija kitakacho boresha maisha ya wakulima na kuwawezesha vijana na wanawake kujiajiri nchini.

“Mradi huu unaenda kufungua njia kwa ajili ya sekta ya kilimo yenye ustahimilivu na jumuishi sambamba na mbinu ya SAGCOT yenye mafanikio kama ilivyoagizwa na Rais Samia Suluhu Hassan, itaigwa katika mikoa mingine nchini kote,” amesema.

Mloge amesema mradi unalenga kongani tano ndani ya Ukanda wa Kukuza Kilimo Kusini mwa Tanzania (SAGCOT) ikiwemo Kongani ya Ihemi, (wilaya ya Iringa, Kilolo, Mufindi na wangingombe), na Kongani ya Mbalali ( Wilaya ya Mbalali).

Mpango huo utatoa fursa ya kuwaelimisha wakulima katika mikoa mbalimbali, ikiwemo Mkoa wa Pwani, Morogoro, Dodoma, Singida, Shinyanga, Simiyu, Geita, Mwanza, na Kigoma. Kwa msaada kutoka kwa wadau wa CARE na SAGCOT,