Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Daniel Godfrey Chongolo leo Ijumaa Oktoba 6, 2023 amekagua Skimu ya Umwagiliaji ya Ugalla katika Kijiji cha Katambike, wilayani Mpanda, ili kuuwekea mpango wa kuukwamua, baada ya mradi huo kukwama tangu 2007.

Ndugu Chongolo amefanya ukaguzi wa skimu hiyo iliyogharimu zaidi ya shilingi milioni 800 wakati wa ziara ya kuimarisha uhai wa chama, kusikiliza kero za wananchi na kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025 katika Halmashauri ya Nsimbo, Wilaya ya Mpanda, Mkoa wa Katavi.

Akizungumza na wananchi wa maeneo ambao ndiyo walikuwa walengwa na wanufaikaji wa Skimu ya Umwagiliaji hiyo inayotegemea maji ya Mto Ugalla, amesisitiza kuwa mradi huo unapaswa kufanya kazi ili wakulima wa maeneo hayo waendelee kufanya kilimo na kuzalisha zaidi ya sasa, ambapo amesema atamuita Waziri wa Kilimo Hussein Bashe ili kupata mpango wa wizara katika maeneo hayo ukoje, kwa ajili ya uukwamua mradi huo uliokwama kwa miaka 16 tangu uanzishwe.

“Mradi huu wa skimu ya umwagiliaji umekwama tangu mwaka 2007. Zinatajwa tu fedha hapa, ziliingia zikaingia, lakini watu wanawashangaa kuwa hizo fedha zilienda wapi? Nitakwenda kuzungumza na Waziri mwenye dhamana na Kilimo ili aone namna ya kuukwamua mradi huu ambao tija yake ni kubwa endapo utafanya kazi,

Akiwa katika eneo hilo Chongolo amesisitiza kuwa mradi huo inatakiwa ufanyike usanifu wa kina unaoendana na mazingira husika, ili upatikane mradi ambao utakua endelevu na wa uhakika.

By Jamhuri