Na Mwandishi wetu, JAMHURI MEDIA

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia Afya Dkt. Charles Mahera amewataka wahudumu wa afya kuwa na kauli nzuri kwa wagonjwa pia amewaagiza watendaji wote katika Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kutunza vifaa vya afya vilivyonunuliwa na Serikali ili viweze kudumu na kuweza kutoa huduma kwa jamii.

Ametoa kauli hiyo Machi 30, 2023 katika ziara ya kukagua utoaji wa huduma, miundombinu ya hospitali, vifaa na shughuli zinazoendelea katika hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu Mangaka.

Amesema Serikali imenunua vifaa kwenye vituo vyote vya kutolea huduma za afya ili kuboresha utoaji wa huduma kwa jamii vikiwemo vifaa vya x-ray mashine, ultrasound mashine na vyengine hivyo, kama watendaji na wasimamizi wanawajibu wa kuvitunza, kuvihudumia na kuhakikisha huduma zinazotolewa ziende sambamba na utoaji wa huduma bora kwa jamii.

“Mnafanya kazi ya Mungu ni vizuri kauli zenu kwa wagonjwa ziwe nzuri Serikali inatambua umuhimu wenu na majukumu yenu”amesema Dkt. Mahera

Ametoa wito kwa watoa huduma za afya nchini kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uadilifu kwa kuwa Serikali inatambua changamoto zinazowakabili.

Dkt. Mahera amesema Serikali itaendelea kushughulikia changamoto zilizopo kwenye sekta ya afya na amewataka kuhakikisha wanaweka mifumo ya ukusanyaji wa mapato “GoTHomis” katika vituo vyote ili mapato hayo yaweze kusaidia kuendeleza utoaji wa huduma bora za afya katika hospitali hizo.

Akitoa taarifa Mganga Mkuu wa Halmashauri Wilaya na Nanyumbu Dkt. Raphael Mhana ameishukuru Serikali kwa kuendelea kununua vifaa na vifaa tiba ili kuboresha sekta ya afya na kuiomba kuendelea kupunguza changamoto ya uhaba wa watumishi katika sekta ya afya.

Aidha, Dkt. Mhana amesema hospitali hiyo ni kongwe katika Halmashauri hiyo, hivyo ameiomba Serikali kuiangalia ili wananchi wa Halmshauri hiyo waweze kupata huduma muhimu na zinazojitosheleza.

By Jamhuri