Na Mwandishi Wetu,Tanga

Waziri wa Afya Ummy Mwalimu ametembelea majeruhi wa ajali ya gari iliyobeba gesi na kudondoka eneo la Kwamkono wilayani Handeni mkoani Tanga ambao wamelazwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo.

Baada ya majadiliano na Mganga Mfawidhi wa Hospital ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo Dkt Naima Yusuf alishauri wapewe Rufaa kwenda Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu kutokana na kwamba ina sehemu maalumu ya kutibu wagonjwa walioungua.

Gari hilo ambalo lilikuwa limebeba gesi baada ya kudondoka gesi hiyo iliweza kusambaa na kutapakaa kwenye maeneo mbalimbali katika eneo hilo na hivyo kusababisha madhara hayo makubwa kwa wananchi ikiwemo baadhi yao kuungua.

Aliongozana na Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo Dkt.Naima Yusuf na Katibu wa Afya Mkoa wa Tanga Frank Mhilu alipata fursa ya kuwatembelea wagonjwa wengine pia na kuwajulia hali huku akiwapongeza wauguzi na madaktari kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuwahudumia wananchi wanaokwenda kupata huduma kwenye hospitali hiyo.

Akizungumza kuhusu majeruhi wa ajali ya gari la gesi lililoungua eneo la kwamkono wilayani Handeni ,Waziri Ummy alisema kutokana na kwamba hali zao kutokuwa nzuri hivyo upo umuhimu wa kupewa rufaa na kupelekwa kwenye hospitali ya Taifa ya Muhimbili ili kuweza kupata huduma Zaidi.

“Kutokana na hali zao kutokuwa nzuri ninashauri majeruhi hao wapewe rufaa na kupelekwa kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya matibabu Zaidi”alisema.

Hata hivyo Waziri Ummy alisema kwamba wanaangalia uwezekano wa kulifanyia ukarabati Jengo la Clief ambalo lipo kwenye hospitali hiyo ili liweze kuwa na muonekana mzuri tofauti na lillivyokuwa hivi sasa.

By Jamhuri