Dkt.Samia anunua magari 727 ya kubebea wagonjwa

Na WAF- Dodoma

NAIBU Waziri wa afya Dkt.Godwin Mollel amebainisha kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha za kununua magari ya kubebea wagonjwa (Ambulance) 727 zitazosaidia kurahisisha huduma za rufaa nchini.

Dkt.Mollel amesema hilo leo Februari 09, 2023 wakati akijibu swali la Stella Manyanya katika Mkutano wa kumi kikao cha nane, Bungeni Jijini Dodoma.

Amesema, katika kuboresha hospitali ya Rufaa ya kanda ya kusini, tayari Serikali imetoa jumla ya shilingi Bilioni 4.4 itayosaidia kujenga majengo ya nyumba za wafanyakazi, ujenzi wa chumba cha kuhufadhia maiti, umaliziaji wa maabara na umaliziaji wa jengo la mama na mtoto.

Sambamba na hilo, Dkt. Mollel amesema, Serikali inaendelea kuboresha huduma nchini, na tayari Serikali imeanza kupeleka madaktari bingwa katika hospitali ya Rufaa ya kanda ya kusini, huku vifaa kama CT-SCAN pamoja na MRI vikiwa tayari vimefungwa tayari kuanza kutoa huduma.