Jumla ya watu 251 wamepata huduma ya upimaji wa viashiria vya magonjwa ya moyo pamoja na ushauri wa jinsi ya kuepukana na magonjwa hayo kutoka kwa wauguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Upimaji huo ulifanyika katika maadhimisho ya miaka 70 ya Baraza la Uuguzi na Ukunga yaliyoenda sambamba na maonesho ya siku tatu ya huduma zinazotolewa na wauguzi yaliyomalika jana katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Akitoa taarifa ya upimaji uliofanyika katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mlollel, Mkurugenzi wa Uuguzi wa JKCI Robert Mallya amesema katika banda hilo huduma zilizokuwa zinatolewa ni upimaji wa kiwango cha sukari mwilini, shinikizo la damu, kueleza huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa, kutoa elimu ya lishe bora na jinsi ya kuepukana na magonjwa ya moyo.

Mkurugenzi wa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Robert Mallya akimweleza Naibu Waziri wa Afya Dkt.Godwin Mollel huduma za matibabu ya moyo zilizotolewa katika banda la Taasisi hiyo wakati wa
maadhimisho ya miaka 70 ya Baraza la Uuguzi na Ukunga yaliyoenda sambamba na maonesho ya siku tatu ya huduma zinazotolewa na wauguzi yaliyomalizika jana katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma

Mallya amesema kati ya watu 251 waliowafanyiwa vipimo 64 walikuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu ambapo 41 kati yao hawakuwa wanajijua kabisa kuwa na tatizo hilo na 23 walikuwa wanajijua na wanatumia dawa .

“Kwa wale ambao hawakuwa wanajijua kuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu tumewashauri waende katika Hospitali za karibu na wanapoishi kwa ajili ya kuanza matibabu na ambao wanajijua tumewashauri wasiache kutumia dawa hata kama watajisikia wanaendelea vizuri.

“Tumetoa elimu ya lishe bora kwa wananchi waliotembelea katika banda letu hii ikiwa ni pamoja na kuepuka kula vyakula vyenye chumvi na mafuta mengi, wasipende kula na kunywa vinywaji vilivyosindikwa kwani vinamadhara katika afya ya moyo”, amesema Mallya.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel amewapongeza wauguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kutoa huduma ya upimaji na ushauri wa magonjwa ya moyo kwa wananchi na kuwataka kuendelea kutoa huduma hiyo pindi wanapopata nafasi ya kufanya hivyo.

“JKCI inatoa huduma nzuri ya matibabu ya moyo kwa wagonjwa wanaowatibu na kwa wananchi wanaowahudumia katika maeneo mbalimbali hapa nchini, ninawaomba muendelee kutoa huduma hii nzuri ili isitokee Hospitali nyingine ikawashinda katika utoaji wa huduma bora ya matibabu ya moyo hapa nchini”, alisisitiza Dkt. Mollel.

Jumla ya Taasisi na Hospitali za serikali na binafsi 26 zilishiriki katika maonesho hayo ambapo kauli mbiu ya maadhimisho ya miaka 70 ya baraza la uuguzi na ukunga ilikuwa ni Bima ya Afya kwa Wote Muuguzi na Mkunga Tarajio la Huduma Bora kwa Jamii.

By Jamhuri