Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Bagamoyo

HALMASHAURI ya wilaya ya Bagamoyo, Mkoani Pwani inakabiliwa na changamoto ya upungufu wa madawati 7,000 katika shule za msingi na sekondari.

Kutokana na mahitaji ya madawati hayo inahitajika kiasi cha sh.milioni 350 ili kuondokana na tatizo hilo.

Akitoa ufafanuzi huo katika baraza la madiwani, utekelezaji wa kata kwa kata kipindi cha miezi mitatu January hadi march, baada ya diwani wa Kata ya Magomeni ,Mwanaharusi Jarufu ,kutaka kujua ufumbuzi wa changamoto ya madawati kwenye baadhi ya shule, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bagamoyo, Shauri Selenda alisema, kero hiyo inashughulikiwa.

“Shule za msingi mahitaji ni madawati 3,000 na sekondari uhitaji ni madawati 4,000 jumla yanatakiwa karibia madawati 7,000 na milioni 350 zinahitajika kumaliza tatizo “alieleza Selenda.

Alieleza, halmashauri imechukua hatua na ilitenga milioni 100 ambayo haitoshelezi inahitajika milioni 350.

Selenda aliomba wadau wa maendeleo, kuendelea kuunga mkono utatuzi wa suala hilo kwa kujitokeza kumaliza kero hiyo.

Kadhalika akielezea juu ya dampo la Magomeni, Selenda alieleza ,wanaangalia namna ya kulihamisha eneo jingine ili kuliondoa katikati ya Mji na eneo la makazi ya watu.

“Wilaya inakua,dampo lipo eneo la makazi, kwasasa tunaangalia namna ya kulihamisha kulitoa katikati ya Mji “

Kuhusu changamoto ya barabara nyingi kuharibika kutokana na mvua zilizonyesha kipindi kirefu, Meneja wa TARURA Bagamoyo, Mhandisi Angetile Bupe alieleza, hali ya hewa inaanza kuwa shwari wanatarajia wakandarasi kurejea kazini kufanya maboresho na wengine kuendelea na ujenzi.

“Hali ya mvua ilisababisha wakandarasi kusimamisha kazi zao, barabara nyingine nyingi zimeharibika kutokana na mvua kubwa,lakini wanatarajia kuendelea na kazi zao “alieleza Bupe .

Bupe alieleza, kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2023/2024 TARURA ilitenga bilioni 2.112 kwa ajili ya utekelezaji mbalimbali wa miundombinu ya barabara, mikataba inayotekelezwa ni sita bado milioni 703 ya mikataba mitatu ambazo hawajazipokea.

Awali katika baraza hilo, Mrisho Saidi amekula kiapo cha kisheria, kuwa Diwani rasmi wa kata ya Fukayosi, Diwani ambae ameshika nafasi ya marehemu Ally Ally Issa aliyefariki dunia aliyefariki dunia Novemba 2023.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo, ambae ni Diwani wa kata ya Yombo Usinga alisema , Diwani wa Fukayosi ataendelea kwenye Kamati ya uchumi, ujenzi na Mazingira.