Mwamvua Mwinyi, JanburiMedia,Pwani

Kanda ya Mashariki , mikoa minne ya Pwani, Dar es Salaam, Morogoro na Tanga, imedhamiria kuwa Kanda ya Mfano katika uwekezaji kutokana na uwepo wa Fursa nyingi kwenye sekta ya kilimo,mifugo, na uvuvi.

Dhamira hiyo inakwenda sambamba na kuinua sekta hizo kwa kutumia teknolojia mpya za kisasa ili kuongeza tija kwa jamii.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu ufunguzi wa Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki, yatakayofanyika Morogoro Agost 1 hadi 8 mwaka huu ,Mkuu wa Mkoa wa Pwani alhaj Abubakari Kunenge alieleza maonyesho hayo yatafunguliwa na Mizengo Kayanza Peter Pinda Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Amesema, maonyesho haya ni ya 30 tangu kuundwa kwa Kanda hiyo mwaka 1993.

Ameeleza, mwaka huu 2023 wadau wamejitokeza kwa wingi 589 sawa na ongezeko la asilimia 22 kutoka wadau 476 wa mwaka 2022.

Kunenge alieleza kuwa, kauli mbinu ya mwaka huu vijana , wanawake ni msingi imara ya uendelevu wa chakula,kwani mchango wa vijana na wanawake unatambuliwa katika kuimarisha chakula matumizi ya chakula.

“Kauli mbinu hii inaendana na jitihada za Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan,ambae anahimiza kuongeza uzalishaji wa chakula kulisha Bara letu na Dunia.

Kunenge aliwaomba wananchi wajitokeze kwa wingi ili kujionea teknolojia mbalimbali za kisasa kuongeza uzalishaji na tija kupitia Ufugaji,Uvuvi na Kilimo.

“Kanda ya Mashariki ni kanda inayokuwa kwa kasi ni kanda ya Kiuchumi, na hayo yote yatawezekana na kuweza kuakisi matokeo ya kila siku na kuongeza tija “anafafanua Kunenge.

By Jamhuri