Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amesema suala la Madaktari Bingwa kufanya kazi ya Kliniki binafsi katika Hospitali za umma baada ya saa za kazi sio jipya na tayari linafanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, JKCI, Ocean Road na Taasisi ya Mifupa MOI ambapo lilianza kutekelezwa zaidi ya miaka 15 iliyopita (IPPM-Intramural Private Practice).

Waziri Ummy amesema lengo ni kutoa muda zaidi kwa wananchi kuweza kupata huduma za matibabu ya kibingwa kutoka kwa wataalam hao na pia kutoa motisha kwa kuongeza kipato cha madaktari bingwa na bobezi walioajiriwa na Serikali.

“Kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali kwenye Sekta ya Afya, sasa tunataka kushusha utaratibu huu kwenye Hospitali za Rufaa za Mikoa ili kubakiza Madaktari bingwa waendelea kufanya kazi mikoani, hili jambo lina tija katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za kibingwa Mikoani, Daktari bingwa anapata na Hospitali inapata, muhimu kuweka utaratibu mzuri na wa wazi” amesema Waziri Ummy.

“Tuna uhaba wa Madaktari bingwa katika Hospitali za Rufaa za Mikoa, Mwezi uliopita tulitangaza nafasi 35 walioomba ni 15 tu, kama Wizara tutaendelea kuweka mikakati mbalimbali ili kuvutia Madaktari bingwa kufanya kazi katika Hospitali za umma hasa za Mikoani” amefafanua Waziri Ummy.

Waziri Ummy amesema kuwa utaratibu huo utawezesha utoaji wa huduma kwa wagonjwa wanaohitaji kuhudumiwa kwa uharaka na kuwatuliza Madaktari kwenye vituo vyao vya kazi na kuwapunguzia adha ya kukimbia kwenye vituo binafsi(maarufu vijiwe au vioski) baada ya muda wa kazi.

“kukimbia kimbia maeneo tofauti hii kunashusha heshima ya kitaaluma kwao na wengine kulazimika kufanya kazi katika mazingira hatarishi na yenye uwekezaji mdogo wa miundo mbinu na vifaa Tiba kuliko alivyoviacha katika Hospital yake ya Rufaa ya umma” amefafanua Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy amebainisha kuwa utaratibu huo utaongeza mapato ya Hospitali za Rufaa za Mkoa. “Mapato yatasaidia kuongeza faida na uwekezaji utakaowafaidisha wagonjwa wote, unachangia kuwezesha hospitali kuhudumia wagonjwa wa msamaha, kuongeza motisha kwa watumishi wote kutokana na mapato hayo ambayo hugawanywa wa watumishi wote wa Hospitali husika

By Jamhuri