Mafanikio yoyote yana sababu (11)

Na Padre Dk. Faustin Kamugisha

 

Shukrani ni sababu ya mafanikio. “Kama unataka kugeuza maisha yako, jaribu kushukuru. Maisha yako yatabadilika kwa kiasi kikubwa sana,” alisema Gerald Good. Ingawa tuna mioyo midogo, lakini inaweza kubeba jambo kubwa nalo ni shukrani. Hesabu mafanikio usihesabu matatizo. Hesabu baraka, usihesabu balaa. “Afadhali kupoteza hesabu wakati unahesabu baraka zako kuliko kupoteza baraka wakati unahesabu matatizo yako,” alisema Maltibie D. Babcock (1858–1901) mwandishi wa vitabu.

Rhonda Byrne katika kitabu chake The Magic ameiita shukrani “uchawi” wa kukufanya ufanikiwe. Anaona shukrani kama siri kubwa ya mafanikio. Baadhi ya nukuu kutoka katika kitabu chake ni kama ifuatavyo: “Shukrani yako ni ya kisumaku, unapokuwa na shukrani zaidi, unavuta kisumaku vitu zaidi.”  Pia aliandika, “Unapokuwa na shukrani kwa vitu ulivyo navyo, hata vikiwa vichache, utaona vitu hivyo vinaongezeka mara.” Kuwa na shukrani kwa vitu ulivyo navyo ni pamoja na kuvithamini.

Shukrani ni ufunguo wa mafanikio. Shukrani inafungua milango mingi ambayo imefungwa. “Shukrani inafungua maisha tele. Inageuza tulichonacho ambacho hakitoshi kinatosha na kuzidi. Inabadili kukataa kunakuwa kukubali, fujo inakuwa utaratibu, kutoeleweka na kuwa kuweleweka. Inageuza mlo kuwa sikukuu, jengo kuwa nyumba, mgeni usiyemjua kuwa rafiki. Shukrani inayapa maana yaliyopita, inaleta amani kwa leo na kuumba maono kwa ajili ya kesho,” alisema Melody Beatrice.

Ni katika msingi huu Wahaya wana methali isemayo: Asiyeshukuru hupewa mara moja- Entasima ehabwa limoi. Bila shukrani hakuna nyongeza. “Tunapotoa kwa furaha na kupokea kwa shukrani, kila mtu anabarikiwa,” alisema Maya Angelou (1928 -2014) aliyepata tuzo kwa kitabu cha kumbukumbu: I Know Why the Caged Bird Sings.

Katika shida jaribu kushukuru. Kuna mtu aliitwa Ayubu alikuwa tajiri sana, aliishi mahali palipoitwa Uz. Alipata habari kuwa amepoteza watoto na mifugo sababu ya maafa na matendo ya wavamizi. Utajiri wake ulitoweka. Aliposhukuru alitendewa makuu. Alisema: “Bwana ametoa Bwana ametwaa, jina lake litukuzwe.” Alikuwa tajiri tena.

Helen Keller ambaye alikuwa ni kiziwi, kipofu na bubu aliandika, “Nimepewa mambo mengi! Sina muda wa kufikiria juu ya yale ambayo sikupewa.” Alikuwa na moyo wa shukrani. Mungu alimpa mengi zaidi kama elimu, kipawa cha kuandika vitabu ingawa alikuwa kipofu, kiziwi na bubu. Hellen Keller aliandika: “Kila mara nimefikiria ingekuwa baraka kama kila mtu angekuwa kipofu na kiziwi kwa siku chache wakati wa siku zake za kwanza za utu uzima. Giza lingemfanya akiri uzuri wa mwanga; ukimya ungemfundisha furaha ya sauti.”

Kuna vitu ambavyo tunavyo, lakini hatukiri uzuri wake na umuhimu wake mpaka tumevipoteza. “Hatuna budi kupata muda wa kutulia na kushukuru watu ambao wameleta tofauti katika maisha yetu,” alisema John F. Kennedy.

Kuna hadithi juu ya mtu aliyegundua ghala ambapo Shetani hutunza mbegu zake tayari kwa kupandwa kwenye moyo wa binadamu. Aligundua mbegu za kukatisha tamaa zilikuwa nyingi sana kuliko mbegu nyingine. Alijifunza kuwa mbegu hizo zilifanywa kuchipuka karibu kila mahali. Shetani alipoulizwa juu ya mbegu za kukatisha tamaa kuweza kuchipuka kila mahali, alisita kidogo na kukiri kuwa kuna sehemu ambapo haziwezi kuchipuka. “Wapi?” aliuliza mtu huyo. Shetani alijibu kwa huzuni, “Katika moyo wa mtu mwenye shukrani.”

Ukiwa mtu mwenye shukrani si rahisi kukatishwa tamaa. Ukiwa mwenye shukrani utakuwa mtu wa furaha. “Hautaona kamwe mtu mwenye furaha asiye na shukrani,” alisema Zig Ziglar. Omba kuwa na moyo wenye shukrani, kama sala aliyotunga George Herbert, “Ee Mungu, wewe ingawa umetupa vitu vingi, tunaomba utuonee huruma utupe jambo moja zaidi- Moyo wenye shukrani.”