Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Kilosa

Jumla ya watu 1404 wameathirika na mafuriko ya mvua zinazoendelea kunyesha katika Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro na nyumba 351 zimeingia maji pamoja na vyoo 368 vimebomoka.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Shaka Hamdu Shaka, kuwa kaya zilizoathirika ni 368 na nyumba 17 zimebomoka.

Alisema kitongoji cha Kampala kaya 161 na watu 624 wameathirika, Kitongoji cha Madizi kaya 137 zimeathirika na watu 531, Kitongoji cha Estate kaya zilizoathirika 57 na watu 196 wameathirika.

Kitongoji kingine ni cha Lugunga kata nane na watu 32 wameathirika, Kitongoji cha PWD kaya tano na watu 20 wameathirika.

Shaka amesema nyumba 17 zilizobomoko tano zinatoka kitongoji cha Kampala, nyumba nane kitongoji cha Estate na nyumba nne kitongoji cha Madizini.

Alisema jumla ya vyoo 368 vimeathirika kutokana na mafuriko, hivyo kufanya maji kuwa machafu baada ya vyoo hivyo kutapishwa na mafuriko baada ya kubomoka.

Aidha, Shaka amesema jumla ya visima 30 vya maji vinavyotumika vimeathirika na mafuriko hayo kwa kuingiliwa na maji machafu.

Akizungumzia kuhusina na hali ya miundombinu ya barabara, Shaka alisema zaidi kilometer 170 za barabara ya imeathirika kwa maji kukata barabra na kusababisha kukatika kwa mawasiliano baina ya Kilosa na Mikumi maeneo mengine ya yanayounganisha vijiji na vijiji hali iliyosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi na shuhuli za usafirishaji bidhaa.

Amesema Machi 17 mwaka huu maji mengi yalijaa katika mto Miyombo unaopita katika vijiji vya Ulaya, Zombo na Changarawe baada ya mvua kubwa kunyesha katika vijiji vya Kisanga, Madizini na Kitunduweta.

Amefahamisha kuwa mvua hiyo ilisababisha athari katika makazi, mashamba na miundombinu ya maji na barabara katika maeneo hayo.

Shaka alifafanunua kuwa kijiji cha Changarawe kimekuwa na matukio ya kupatwa na mafuriko mara kwa mara tangu mwaka 2016 na msimu huu wa mvua tangu Desemba mwaka jana hadi sasa ni tukio la tisa la mafuriko.

“Mafuriko haya yamesababishwa na maji kujaa katika mto Miyombo nje ya kingo za mto baada ya ongezeko la kujaa mchanga katika mabwawa ya Nara na Kipera ambayo yalichimbwa kwa ajili ya kupunguza kasi ya maji kipindi cha mvua kubwa na kuruhusu maji machache kuingia katika mto huo,”alisema Shaka.

Shaka amebainisha kuwa uharibifu wa tuta hilo lililojengwa pia kuzuia maji yasiingie katika mashamba ya mkonge enzi hizo kwa sasa yamekuwa ni makazi ya watu.

Aidha, amesema shughuli za kibinadamu katika kingo za mto huo ambapo wakazi wa eneo hilo hulima na kuchunga katika tuta hilo wameathiriwa na mvua hizo.

Katika hatua ingine Shaka amemshukuru Dkt Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoguswa na hali ya mafuriko katika Wilaya hiyo ambapo nyakati zote amekuwa akielekeza hatua mbali mbali za haraka na dharura ili kuokoa maisha ya wananchi lakini pia kurudi huduma za kibinadamu.

“Tangu Desemba hadi leo tumekuwa na mafuriko ya mara kwa mara Mheshimiwa Rais Samia amekuwa nasi nyakati zote tumepokea msaada wa chakula cha dharura, matibabu, magodoro lakini pia fedha za mfuko wa dharura katika kurudisha miundombinu ya barabara wananchi wanamsuhkuru sana rais” amesema.

By Jamhuri