Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameagiza watumishi wa Halmashauri ya wilaya Mlele wahamie mara moja kwenye nyumba 11 zilizokuwa za wajenzi wa barabara ya Inyonga-Mlele na kukabidhiwa kwa Halmashauri hiyo.

Watumishi ambao ameagiza wahamie kwenye nyumba hizo ni Afisa Usalama wq Wilaya (DSO), Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Mlele (OCD), Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mlele, Meneja wa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mlele (DMO) pamoja na watumishi wengine wa hospitali ya wilaya.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza  na watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Mlele akida katika zira ya Mkoa wa Katavi.

Waziri Mkuu alitoa agizo hilo jana Desemba 13, 2022 wakati akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Mlele mkoani Katavi baada ya kujionea mwenyewe kuwa zimetelekezwa na zinaharibika kwa kukosa uangalizi.

“Watumishi wanahangaika hawana makazi, nyumba zimeachwa nyasi zimeota hadi kwenye korido. Watumishi wote wanaopaswa kuhamia katika nyumba hizi baada ya kumaliza mkutano huu kila mmoja aende kwenye nyumba yake na ahamie,” amesema.

Nyumba hizo 11 zenye ukubwa tofauti kati yake mbili zinauwezo wa kuchukua familia nne kila moja ni za kisasa na zilikabidhiwa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mlele Novemba 2022 na Wakala wa Barabara Tanzania {TANROADS} baada ya kukamilika kwa mradi wa barabara.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Mlele akiwa kwenye ziara ya Mkoa wa Katavi, Disemba 13, 2022. Katikati ni Kaimu  Mkuu wa Mkoa wa Rukwa na  Mkuu wa wilaya ya Tanganyika, Onesmo Buwelu na wa  pili kulia ni Katibu Tawala wa mkoa wa katavi, Hassan Rugwa. 

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa ameutaka uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mlele uweke utaratibu wa kushirikisha wadau wa sekta binafsi katika kuleta maendeleo kwenye wilaya yao. Pia aliwataka watumishi hao wahakikishe kila kazi wanazozifanya zinakuwa na matokeo chanya kwa jamii.

Awali, Waziri Mkuu alikagua barabara ya lami ya Inyonga-Mapili yenye urefu wa kilomita 11.7 iliyogharimu shilingi bilioni 8.69. Barabara hiyo ni sehemu ya barabara ya Inyonga-Ilunde-Kishelo inayokwenda hadi kwenye mpaka wa mkoa wa Katavi na Tabora ikiwa na urefu wa kilomita 96.

Wakizungumza baada ya ukaguzi huo, baadhi ya wakazi wa eneo la Mapili walimshukuru Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo ambayo kukamilika kwake kutaimarisha huduma za usafiri wa watu na mizigo.

Baadhi ya watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Mlele wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipozungumza nao akiwa kwenye zira ya Mkoa wa Katavi.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi katika kijiji cha Mapili wilayani Mlele baada ya kukagua barabara ya lami  ya Inyonga – Mapili yenye urefu wa kilimita  8.69, Desemba 13, 2022. Alikuwa katika ziara ya Mkoa wa Katavi. 
Muonekano wa barabara ya lami  ya Inyonga – Mapili yenye urefu wa kilomita  8.69 ambayo Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alikagua ujenzi wake
Baadhi ya wananchi wakimsikiliza Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati alipowahutubia  katika kijiji cha Mapili wilayani Mlele akiwa katika ziara ya Mkoa wa Katavi.

By Jamhuri