Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia Mlele

Mbunge wa Jimbo la Kavuu katika halmashauri ya Mpimbwe mkoa wa Katavi na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe, Geophrey Pinda amekabidhi majiko mia mbili ya Gesi ya kupikia kwa taasisi na vikundi mbalimbali katika jimbo lake.

Mhe, Pinda alikabidhi majiko hayo tarehe 25 Februari 2024 mara baada ya Mkutano Mkuu wa jimbo la Kavuu Kuwasilisha Taarifa ya Utekelezaji Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuanzia Novemba 2020 hadi Februari 2024. Mgeni rasmi kwenye mkutano huo alikuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Kassim Majaliwa Majaliwa.

Taasisi na vikundi vilivyokabidhiwa majiko hayo ya gesi ya kupikia ni pamoja na Shule za Msingi na Sekondari, Zahanati, Vituo vya Afya na vikundi vya mama lishe.

Mhe, Pinda amesema, uamuzi wa kukabidhi majiko ya gesi kwa taasisi na vikundi mbalimbali una lengo la kuwafikia watu wengi zaidi sambamba kuzifanya taasisi na vikundi kuanza kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.

‘’Nimeamua kukabidhi majiko haya kwa taasisi kama shule, Hospitali pamoja na vikundi mbalimbali kwa kuwa maumizi yake yanahusisha idadi kubwa ya watu tofauti na ningetoa kwa mtu mmoja mmoja’’ alisema Mhe, Pinda.

Kwa upande wa wawakilishi wa shule za Sekondari na msingi walimshukuru Mbunge wa Jimbo la Kavuu kwa uamuzi wa kuwapatia majiko ya gesi na kueleza kuwa majiko hayo yatawarahisshia katika kupika vyakula.

‘’Tukushukuru sana Mhe, Mbunge kwa uamuzi wa kutupatia majiko ya gesi, sasa tutanaweza kupika na kuchemsha maji muda wowote, tunakushukuru’’ alisema Mbunge huyo wa jimbo la Kavuu.

Makabidhiano ya majiko hayo ni sehemu ya shughuli za Mkutano Mkuu wa Jimbo la Kavuu wa kuwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya CCM kuanzia Novemba 2020 hadi Februari 2024 ambapo Mbunge wa Jimbo hilo la Kavuu alieleza mafanikio yaliyopatikana tangu aingie madarakani.

By Jamhuri