Marekani yaonya iko tayari kurejea vitani na Iran, huku Trump akisisitiza masharti makali ya makubaliano ya amani, wakati mazungumzo na mvutano Mashariki ya Kati ukiendelea kuongezeka.

Marekani imesema iko tayari kurejea vitani na Iran ikiwa itahitajika, huku Rais wa Marekani, Donald Trump, akisisitiza kuwa makubaliano yoyote ya amani lazima yaheshimu masharti yake, ikiwemo Iran kutoruhusiwa kamwe kutengeneza silaha za nyuklia.

Kauli hiyo ilitolewa wakati mazungumzo ya kusitisha mzozo wa Mashariki ya Kati yakiendelea. Ingawa Ikulu ya Marekani imeashiria kuwa makubaliano ya awali yako karibu kufikiwa, Iran imesema bado hakuna makubaliano ya mwisho yaliyoafikiwa.

Wakati huohuo, Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth, akiwa katika mkutano mkubwa wa usalama barani Asia nchini Singapore, amesema kuwa Washington inaweza kuanzisha tena vita “ikiwa itaamua kufanya hivyo,” akisisitiza kuwa Marekani ina uwezo na akiba ya kutosha ya silaha.

Kwa upande wake, Iran imekataa masharti yaliyowekwa na Washington. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmaeil Baqaei, amesema nchi hiyo haikubali kuamrishwa kuhusu sera zake.

Huku haya yakijiri, mapigano yanaendelea nchini Lebanon kati ya Israel na kundi la Hezbollah. Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, amesema majeshi ya nchi yake yamesonga mbele zaidi ndani ya Lebanon, huku juhudi za kidiplomasia za kusitisha mapigano zinaendelea.