Na zuena Msuya,JamhuriMediaTanga

Kamati ya kuishauri Serikali namna ya upatikanaji wa Nguzo bora za Umeme za Miti, imesema kuwa nguzo za miti za umeme zenye ukubwa wa mita 13 zinapatikana nchini tofauti na inavyoelezwa na baadhi ya wakandarasi wanaotekeleza miradi mbalimbali ya kusambaza umeme nchini.

Akizungumza kwa niaba ya kamati hiyo, Katibu wa Kamati hiyo Mhandisi Edson Ngabo wa Wizara ya Nishati, amesema kuwa Kamati hiyo imebaini uwepo wa nguzo hizo baada ya kukagua Kiwanda cha Mbao na Nguzo cha Tembo katika Wilaya ya Korogwe na Kiwanda cha Nguzo cha Mua kilichopo katika Wilaya ya Tanga Mjini wakati wa ziara ya Kamati hiyo Februari 6, 2023 mkoani Tanga.

Nguzo zikiwa tayari kuingizwa katika Mtambo wa kuweka dawa katika nguzo za miti za umeme ili kuzidhibiti tayari kwa matumizi, katika kiwanda cha Mua wakati wa ziara ya Wajumbe wa Kamati ya kuishauri Serikali namna ya upatikanaji wa Nguzo bora za Umeme za Miti ya kukagua viwanda vya nguzo na nguzo katika wilaya ya Tanga Mjini, Februari 6, 2023 mkoani Tanga.

Mhandisi Ngabo amesema kuwa, baada ya kukagua nguzo katika viwanda hivyo na kuzungumza na watendaji wa viwanda hivyo Kamati ilibaini kuwa viwanda hivyo vinauwezo wa kuweza kuzalisha nguzo zenye ukubwa wa mita 13, ambazo zinatumika katika kusambaza umeme wa Msongo Kubwa (High Tension) katika baadhi ya maeneo nchini na miti ya kuzalisha nguzo hizo ipo mashambani.

Alifafanua kuwa baadhi ya baadhi ya wakandarasi wamekuwa waishauri Serikali iwaruhusu kuagiza nguzo za mita 13 nje ya nchi hali ambayo inawanyima fursa wafanyabiasha wa ndani waliowekeza fedha nyingi katika kujenga viwanda vya nguzo nchini.

Hata hivyo Ngabo alisema kuwa, licha ya kuwepo kwa nguzo hizo, viwanda husika vinatakiwa kuzalisha nguzo hizo kwa kuzingatia ubora unaotakiwa katika viwango vya kimataifa ili kuwa na fursa ya kuuza nguzo hizo nje ya nchi kwa kuwa zinahitajika kwa wingi.

“Awali nguzo za mita 12 na 13 zilikuwa ni changamoto kubwa kuzipata, lakini baada ya kutembelea viwanda hivi, tumebaini kuwa nguzo hizo zipo nyingi na zinakidhi mahitaji ya nchi hivyo nawashauri wakandarasi kutumia nguzo za ndani ili kuharakisha utekelezaji wa miradi hivyo kwani Umoja wa Wapanda miti ambao ni sehemu ya Kamati hii wamekiri kuwa na nguzo hizo zipo mashambani kwao, lakini katika siku za hivi karibuni hakuna aliyepata maombi ya uhitaji wa nguzo hizo kutoka kwa wakandarasi, alisema Mhandisi Ngabo.

Wajumbe wa Kamati ya kuishauri Serikali namna ya upatikanaji wa Nguzo bora za Umeme za Miti, wakikagua vifaa vya kupima ubora wa nguzo katika kiwanda cha Mbao na Nguzo cha Tembo katika Wilaya ya Korogwe, wakati wa ziara yao ya kukagua viwanda vya nguzo na nguzo katika wilaya hiyo, Februari 6, 2023 mkoani Tanga.

Kamati hiyo imekipongeza Kiwanda cha Nguzo cha Mua kwa kuweza kuzalisha nguzo hizo pamoja na changamoto wanazokabiliana nazo.

Hata hivyo wamemshauri Mkurugenzi wa kiwanda cha Nguzo cha Mua, Badru Issa Badru, kuwapeleka watumishi wake katika Chuo cha Mafunzo ya Misitu na Viwanda vya Misitu, mara kwa mara ili kuwajengea uwezo wa kuzalisha bidhaaa zenye ubora zaidi zitakazo kidhi viwango vinavyotakiwa.

Aidha, Badru ameishukuru Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme nchini (TANESCO) pamoja Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kuendelea kutoa ushauri wa kitaalam katika kiwanda hicho.

Katika Kiwanda cha mbao na Nguzo cha Tembo, Kamati hiyo ilibaini changamoto mbalimbali zinazokikabili kiwanda hicho, ikiwemo kukosekana kwa watalaam, vitendea kazi vya kutosha kudhibiti ubora wa nguzo na kutokuwa na vibali vyote kutoka Shirika la viwango nchini (TBS).

Wamemtaka mmiliki huyo kufanyia kazi changamoto hizo ili aweze kuendelea kutekeleza majukumu yake, kabla ya kuchukuliwa hatua.

Aidha Kamati imemtaka kutunza nguzo zake kwa kufuata taratibu za uhifadhi wa nguzo mara tu baada ya kuzipokea kutoka shambani ili kupata nguzo bora na kuepuka kupata hasara ya nguzo kupinda ambazo hazifai katika miradi ya kusambaza umeme, pia kupoteza ubora wa rasilimali hiyo bila sababu za msingi.

“Kamati haijaridhishwa na mpangilio wa nguzo ndani ya kiwanda hiki, nguzo nyingi zinaharibika hapa kwa kutokuwa na mpangilio mzuri wa nguzo hizo, tumemshauri kufuata taratibu za upangaji wa nguzo na aongeze nguvu kazi katika hili, alisisitiza Ngabo.

Thomas Mbaga Meneja Mdhibiti ubora wa nguzo Wakala wa Nishati Vijijini (REA), akiwaonyesha jambo, Wajumbe wa Kamati ya kuishauri Serikali namna ya upatikanaji wa Nguzo bora za Umeme za Miti ya kukagua viwanda vya nguzo na nguzo katika kiwanda cha nguzo cha Mua katika wilaya ya Tanga Mjini, Februari 6, 2023 mkoani Tanga

Kamati hiyo itaendelea na ziara ya kukagua viwanda vya nguzo vilivyopo katika Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.

Kamati hiyo iliundwa Mwezi Aprili 2022, na Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba wakati alipofanya Mkutano na wadau wa kuzalisha Nguzo za miti za umeme katika Mikoa ya Iringa na Njombe.

Kamati hiyo inaundwa na Wajumbe 14 kutoka katika kila kundi la Wadau wa nguzo za miti za Umeme nchini, Wizara ya Nishati, Makatibu Tawala wa Njombe na Iringa, Wakala wa Nishati Vijijini( REA), Shirika la umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Viwango nchini ( TBS) na wadau wa Mazao ya Miti.

By Jamhuri