πŸ“Œ Ampongeza Rais Samia kinara nishati safi

πŸ“Œ Awataka wananchi wa Msomera kubeba ajenda ya nishati safi

πŸ“Œ Matumizi ya kuni sasa basi Msomera

πŸ“Œ Serikali yagawa majiko banifu na gesi, yagharimu zaidi ya milioni 200

Na Mwandishi Wetu, Msomera

Naibu Waziri wa Nishati Mhe.Judith Kapinga, amewataka wananchi wa Msomera kuhakikisha wanaibeba ajenda ya nishati safi ya kupikia kwa vitendo kuunga mkono jithada za serikali Ili kulinda mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

Mhe.Kapinga ameyasema hayo katika Kijiji cha Msomera wilaya ya Handeni Mkoa wa Tanga kwenye hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu 1500 iliyotolewa na REA na Taifa gesi, ikiwa ni mwendelezo wa juhudi za Wizara ya Nishati kugawa nishati safi ya kupikia kwa watanzania na kuunga mkono jitihada za Rais, Dkt. Samia kufikisha asilimia 80 ya watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga, akikabidhi jiko la gesi kwa mmoja wa wananchi wa Kijiji cha Msomera wilayani Handeni Mkoa wa Tanga wakati wa hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu kwa wananchi wa kijiji hicho Tarehe 17 Mei, 2024

β€˜Ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia ni ya Mhe.Rais mwenyewe na ndio kinara hivyo lazima tumuunge mkono kwa vitendo kwa kuacha kukata miti kwa ajili ya kupikia.” Amesema Mhe. Kapinga.

Amesema ili kupata gunia moja la mkaa inahitajika magogo tani moja hadi mbili kupata nishati ya mkaa, hivyo amewataka wananchi wa Msomera kutumia kuni sasa basi.

Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga, akikabidhi majiko banifu kwa Mkuu wa Wilaya wa Handeni Wakili Albert Msando wakati wa hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu kwa wananchi wa Kijiji cha Msomera wilayani Handeni Mkoa wa Tanga Tarehe 17 Mei, 2024.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Handeni Wakili Albert Msando amesifu jitihada za Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha watanzania wote wanatumia nishati safi ya kupikia na kuwataka wananchi wa Msomera kutumia vema fursa ya majiko banifu na mitungi ya gesi.

Aidha Msando amemshukuru Naibu Waziri wa Nishati Mhe.Kapinga kwa kuwafikishia mitungi ya gesi 1,500 na majiko banifu 1,500 ambapo awali waliomba 1,000, na kuomba uwezekano wa kuongezewa Ili kufikia kaya 3,400 za Msomera

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA Renatus Nkwabi amesema kuwa matakwa ya nishati safi ya kupikia ni ya watanzania wote na ndio maana REA imetoa majiko banifu kuunga mkono Serikali juu ya ajenda ya nishati safi ya kupikia na kuwataka wananchi wa Msomera kuunga mkono jitihada hizo.

Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga, akikabidhi majiko ya gesi kwa Mkuu wa Wilaya wa Handeni Wakili Albert Msando wakati wa hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu katika Kijiji cha Msomera Wilaya ya Handeni mkoani Tanga Tarehe 17 Mei, 2024.

Jumla ya Kaya zaidi ya 3,000 za wilaya ya Msomera zimepatiwa majiko banifu na mitungi ya gesi kuwezesha Kaya za wananchi wenye asili ya Kimasai waliohamia kutoka Ngorongoro kuja Msomera kunufaika na nishati safi ya kupikia, ikiwa ni mpango mkakati wa serikali wa miaka kumi uliozinduliwa hivi karibuni na Dkt.Samia Suluhu Hassan kuhakikisha matumizi ya nishati isiyo safi yanapunguzwa na kulinda mazingira na afya za watanzania.

Naye Meneja Mkuu wa Kampuni ya Taifa gesi ambao ndio waliotoa mitungi ya gesi kwa wananchi wa Msomera Davis Deogratius, wameahidi kuwasogezea huduma karibu wananchi wa Msomera ili kupata nishati safi ya kupikia kwa wakati.

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Wakili Albert Msando akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Msomera wakati wa hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu wilayani Handeni Mkoa wa Tanga Tarehe 17 Mei, 2024

Aidha wamemshukuru Mhe.Naibu Waziri kwa kutimiza ahadi yake ya kugawa nishati safi ya kupikia kwa wananchi wa Msomera na kuongeza kuwa wako Kama wadau wakubwa wa Nishati safi wataendelea kuunga mkono jitihada za serikali kuwapatia wananchi nishati safi ya kupikia

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Wakurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Handeni na Msomera, Madiwani Kamati ya ulinzi na Usalama na wananchi wa wilaya ya Handeni na Msomera.

Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga, akizungumza na wananchi wa kijiji cha Msomera wilayani Handeni Mkoa wa Tanga wakati wa hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu kwa wananchi hao Tarehe 17 Mei, 2024.
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi na Wananchi wa
Kijiji cha Msomera wilayani Handeni Mkoa wa Tanga wakati wa hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu iliyofanyika Tarehe 17 Mei, 2024
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga na Mkuu wa Wilaya ya Handeni Wakili Albert Msando wakimwelekeza mwananchi namna ya kuwasha jiko la gesi wakati wa hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu iliyofanyika Kijiji cha Msomera Wilaya ya Handeni mkoani Tanga Tarehe 17 Mei, 2024