Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Mwanza

Serikali imetoa shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza urejeshaji wa miundombinu ya barabara zilizoharibika maeneo mbalimbali Mkoani Mwanza.

Fedha hizo zimetolewa na serikali kwenda Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Mwanza ili kuanza haraka kazi ya marekebisho miundombinu ya barabara na madaraja ambayo yameharibika kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.

Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza Mhandisi Paschal Ambrose ameyasema hayo wakati alipotembelea na kukagua uharibifu uliotokea kwenye barabara katika Wilaya za Nyamagana na Misungwi ambapo pia ametumia fursa hiyo kukanusha uvumi ulioenezwa kwamba barabara katika eneo la Ng’ombe Wilayani Misungwi ni mbovu na haipitiki na amewataka wananachi kupuuza uvumi huo.

Amesisitiza kuwa Serikali imetoa fedha za dharura ambapo tayari wakandarasi wapo kazini wakiendelea na kazi.

Amesema miongoni mwa barabara zinazofanyiwa marekebisho ni barabara ya kutoka Mwanza kuelekea Musoma eneo la Nyamhongolo ambapo wanarekebisha mfereji ambao umeharibika kutokana na mvua hizo.

Mhandisi Ambrose amewataka wananchi wanaoishi karibu na barabara kuacha kufanya shughuli za kibinadamu kwenye kingo za barabara pamoja na kutupa taka ngumu katika mitaro hali inayosababisha mitaro kushindwa kupitisha maji pindi mvua zinaponyesha.

Naye Mkandarasi anayefanya marekebisho katika maeneo mbalimbali Mkoani Mwanza Mhandisi Stephen Mashauri kutoka kampuni ya ujenzi ya MUMANGI CONSTRUCTION CO. LTD amewaondoa hofu wananchi wanaotumia barabara hizo kwamba zitarekebishwa kwa wakati ili ziweze kupitika muda wote.

Aidha amewataka madereva wa vyombo vya moto kufuata alama zote, za barabarani zilizowekwa na TANROADS ili kuepuka ajali, huku akiwatahadharisha Wananchi wanaoiba miundombinu iliyowekwa barabarani na kwamba watakaobainika watachukulia hatua kali za kisheria.

By Jamhuri