Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Chama cha NCCR- Mageuzi kimewataka wanachama wake wote nchini kuisoma miswaada ya Sheria ya Uchaguzi yote inayotarajiwa kuwasilishwa kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linalotarajia kuanza Novemba mwaka huu.

Pia chama hicho kimesema hakitasusia miswaada hiyo badala yake kitatoa maoni mahali ambapo panahitajika kufanyiwa marekebisho ili kuhakikisha mchakato wa kupata katiba mpya unafanikiwa kwa wakati.

Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaamu na Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Joseph Selasini wakati akizungumza na waandishi wa habari alipokuwa akizungumzia kuhusu suala la Mkataba wa Ubia wa Bandari ya Dar es Salaam na Kampuni ya Dp Word pamoja na Miswaada ya sheria Uchaguzi.

Aidha, Selasini amesema kwamba chama hicho kimejifunza wakati mchakato wa Bunge la Katiba inayopendekezwa la mwaka 2014 ambapo vyama vya upinzani vilisusia mchakato huo jambo ambalo amedai halikua sawa nakwamba hawapo tayari kurudia makosa ambayo yamekigharimu chama na Taifa kwa ujumla.

“NCCR Mageuzi haitaususia Miswaada hii,,sisi tunawataka wanachama wetu waisome ,na Watanzania wote kuielewa,miswaada hii hadi inapelekwa Bungeni imetokana na jitihada zetu kwenye kutoa maoni kwenye kikosi kazi”amesema Selasini ambaye aliwai kuwa mbunge wa Rombo.

Hata hivyo,Selasini amesema chama hicho hakitasusia Chaguzi zozote zitakazofanyika kuanzia mwakani kwenye Chaguzi za Serikali za Mitaa,na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, huku akiwataka wanachama wote wenye sifa ya kuwania uongozi ikiwemo wa kitongoji,kijiji kujiandaa kuwania nafasi hizo.

Katika hatua nyingine, mwanasiasa huyo amezungumzia kuhusu mkataba wa ubia juu ya uendeshaji wa bandari baina ya Tanzania na Kampuni ya DP Word na kusema kuwa chama hicho kinaunga mkono uwekezaji huo ambao ameuta kuwa unatija kwa Taifa.

Selasini ameipongeza Serikali kwa kusikia maoni ya watu mbalimbali kwa kufanya marekebisha maeneo yaliyokuwa yanalalamikiwa na Watanzania.

“Mkataba huu tofauti na IGA ya awali ulipowasilishwa bungeni,tumeona suala la ukomo tuliambiwa miaka 100 sasahivi ni miaka 30 huku kila baada ya miaka mitano inafanyiwa mapitio kuona kama utekelezaji wake unaenda kama ulivyokubaliwa kwenye Mkataba” amesema.

Nakuongeza kuwa “Tumeona suala la msingi la kuundwa kampuni kati ya wazawa na Kampuni ya DP Word juu ya uendeshaji pamoja na TRA kuhusika katika kukusanya mapato bandarini.

Kadhalika, mwanasiasa huyo pia ameishauri Serikali kuunda timu ya wafanyabiashara itakayofuatilia utekelezaji wa mkataba huo ambapo amesema endapo utasimamiwa vizuri utaleta tija kwa Taifa.