Na Byarugaba Innocent, JamhuriMedia, Kibaha

Jumla ya Wanafunzi 192 wakiwemo 44 wa shule ya Sekondari Kibaha Wavulana kati ya 791 wanaonza safari ya miaka miwili ya kidato cha tano na sita hawajaripoti kwenye shule za Serikali za Halmashauri ya Mji Kibaha.

Afisa Elimu taaluma Sekondari wa Edward Jidamva amethibitisha kuwa mpaka Septemba 14,2023 takwimu zinaonesha ni wanafunzi 599 tu wameripoti kuanza masomo na wanafunzi 192 kati yao wanasichana 42 na Wavulana 150 hawajulikani.

“…Zipo sababu lukuki zinazofanya wanafunzi wachelewe na pengine kutoripoti kwenye shule zetu ikiwemo kwenda shule binafsi,kujiunga na Vyuo vya kati na wengine kujiunga na majeshi ” amesema Jidamva.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Protasi Dibogo ametoa wito kwa wazazi na walezi kuziamini shule za Serikali kutokana na uwekezaji mkubwa uliwekwa na Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kujenga miundombinu bora ya Elimu ikiwemo ujenzi wa Maabara za Sayansi, Maktaba, Madarasa, Majengo ya Utawala,Mabweni sanjali na Elimu bure ili kuwafanya watoto kufurahia masomo yao.

Rosemary Msasi,Afisa Elimu Sekondari wa Kibaha Mji ametanabaisha kuwa kando ya kutamatisha tarehe ya kuwapokea wanafunzi wa kidato cha tano tangu tarehe 31 Agosti, 2023 bado wanawapokea hivyo ametoa rai kwa wazazi na walezi kutumia fursa hii kuwaleta wanafunzi ili wasichelewe masomo zaidi

By Jamhuri