Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Arusha

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulika na masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Ummy Nderiananga amewasihi wataalam na wabobezi mbalimbali wa eneo la Ufuatiliaji na Tathmini kuitekeleza dhana hiyo kwa vitendo.

Naibu Waziri Nderiananga ameyasema hayo mapema leo jijini Arusha wakati akitoa hotuba ya kufunga Kongamamno la pili la Wiki ya Kitaifa ya Ufuatiliaji na Tathmini ambapo amesema umefika wakati sasa wa kutekeleza dhana hiyo kwa vitendo, kwa kushirikisha wadau wote muhimu ndani na nje ya nchi.

Aidha, Mhe. Nderiananga Alibainisha kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendeleza juhudi mbalimbali za kuimarisha eneo la Ufuatiliaji na Tathmini, kwa kuboresha mifumo na Miundo ya Utumishi ili kuendana na mahitaji ya sasa ya upimaji wa Utendaji Kazi wa Taasisi za Umma.

“Hii ni pamoja na kukamilisha Sera ya Taifa ya Ufuatiliaji na Tathmini, Kukamilisha Mwongozo wa Kujenga na kutekeleza Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini kuanzia ngazi ya Taasisi ya Umma, Sekta na Kitaifa, Kuoanisha mifumo ya Taarifa za Ufuatiliaji na Tathmini kwa kuunda Mfumo Jumuishi wa Kielektroniki wa Ufuatiliaji na Tathimini (National Intergrated M&E Dashboard).” Alisema

Aliendelea kueleza kuwa mfumo Jumuishi wa Ufuatilijai na Tathmini utawezesha Mifumo mbalimbali ya utoaji taarifa za utendaji kazi Serikalini kusomana.

“Jitihada hizi ziende bega kwa bega na kuboresha mitaala yetu ili tuweze kupata wataalamu wenye weledi katika kusimamia vizuri utendaji wa shughuli mbalimbali za Serikali ikiwemo miradi ya maendeleo.” Alisisitiza Naibu Waziri Nderiananga.

Kwa upande wa Sekta binafsi na wadau mbalimbali wa maendeleo wa ndani na nje ya Tanzania, Naibu Waziri Nderiananga amewashauri kuendelea kuwa na utayari wa kushirikiana na Serikali ili kuongeza ufanisi wa Ufuatiliaji, Tathmini na upimaji wa utendaji na matokeo.

“Kama ambavyo mmeona uzoefu wa nchi mbalimbali, eneo la Ufuatiliaji na Tathmini si la mtu mmoja, hivyo linahitaji ushirikishwaji wa Wadau wote, Serikali yetu ipo tayari kushirikiana na wadau katika kuimarisha Ufuatiliaji na Tathmini ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora wanazostahili na kwa wakati.” Alisisitiza

Kwa upande wake Bi, Joanita Magongo, Mkuu wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathimini wa Taasisi ya Uongozi amesema baadhi ya maazimio yaliyofikiwa ni pamoja na sera ya Taifa ya ufuatiliaji na tathmini ikamilishwe ili kutoa mwelekeo wa utekelezaji wa eneo la ufuatiliaji na tathmini nchini.

Bi, Magongo amesema maeneo hayo ni pamoja na ukamilishwaji wa mfumo jumuishi wa kielektroniki wa ufuatiliaji na tathmini (Intergrated National M&E System) mfumo ambao umependekezwa uwe na uwezo wa kupokea maoni na kutoa mrejesho kwa wadau.

Ameongeza kuwa maandalizi ya mfumo huo yaende sambamba na maandalizi ya mkakati wa mawasiliano kwa ajili uelewa wa kina kwa wadau.

“Taasisi zote za Serikali ziimarishe Vitengo vya ufuatiliaji na tathmin kwa kuhakikisha vinapatiwa rasilimali za kutosha ili kuwezesha kutekeleza majukumu yao kikamilifu na kuongeza ufanisi,” alisema Bi, Magongo.

Aidha, amesisitiza kuwa serikali iendelee kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutekeleza jukumu la Ufuatiliaji na Tathmini sambamba na taarifa za ufuatiliaji na tathmini kuandaliwa na kujadiliwa katika sekta husika kila robo mwaka.

Kongamano la Pili la Wiki ya Kitaifa ya Ufuatiliji na Tathmini lililofanyika kwa siku nne Jijini Arusha, lilihusisha washiriki mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi, ambapo mada mbalimbali za kitaalamu ziliwasilishwa na Tuzo na vyeti vya Pongezi vilitolewa kwa washiriki mbalimbali.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Ummy Nderiananga akitoa hotuba ya Kufunga Kongamano la Pili la Wiki ya Kitaifa ya Ufuatiliaji na Tathmini wa shughuli za Serikalini iliyofanyika Jijini Arusha.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Ummy Nderiananga akisalimiana na Mkurugenzi wa Idara ya Ufuatiliaji na Tathimini Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Bi, Sakina Mwinyimkuu.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. Ummy Nderiananga akiwa katika picha ya pamoja na wanadiplomasia waliowakilisha nchi zao katika Kongamano la Pili la Wiki ya Kitaifa ya Ufuatiliaji na Tathmini wa shughuli za Serikalini iliyofanyika Jijini Arusha.

By Jamhuri