Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutunza misitu ili iweze kuleta fursa katika uwekezaji wa hewa ya ukaa.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo akiteta na wawekezaji wa hewa ya ukaa kutoka Kampuni ya Relevant Co.Ltd. Bw. Mohamed Sinan na Bw. Abdulrahman Sinani mara baada ya kikao cha kujadili namna ya kushirikiana na Serikali katika uwekezaji huo.

Ametoa wito huo leo Agosti 15, 2022 alipokutana na wawekezaji wa hewa ya ukaa pamoja na timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais jijini Dar es Salaam kujadili namna ya kushirikiana katika uwekezaji huo katika kusaidia utunzaji wa mazingira.

Katika kikao hicho kilichohudhuriwa na wawekezaji hao wa Kampuni ya Carbon Market Exchange kutoka Marekani na Relevant Co.Ltd. ya nchini Tanzania, Waziri Jafo kupitia biashara ya hewa ya ukaa ana imani italeta manufaa kwa mazingira na uchumi.

Alisema suala la ukataji miti kwa ajili ya kuni na mkaa limekuwa kubwa na kuwa takwimu zinaonesha takriban ekari laki nne zinapotea hivyo hatuna budi kuendelea kupanda miti na kulinda misitu.

“Ni matarajio yetu kuwa kikao hiki kimefungua wigo wa mjadala kuhusu namna gani biashara ya hewa ya ukaa inaweza kuwa na manufaa na hata bajeti ya nchi yetu katika miaka inayokuja inawezekana tukawa na mapato makubwa kutokana na biashara ya hewa ya ukaa,” amesema.

Aidha, Waziri Jafo alisema kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imekuwa ikichukua hatua za kukabiliana na athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi.

Pia amesema kuwa miradi ya Kimkakati ya Treni ya Umeme (SGR), Mradi wa Umeme wa Maji wa Mwalimu Nyerere na Mradi wa Mabasi yaendayo kasi (BRT) imekuwa ni miradi ya mfano kimataifa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa upande Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Carbon Market Exhange Bi. Shenna Forthers amesema wanatarajia kupata ushirikiano kutoka Relevant Co.Ltd na Serikali ili kuweza kufanikisha azma ya utunzaji mazingira.

Bi. Forhers aliongeza kuwa uwekezaji huo mbali ya kutumia misitu pia unatarajiwa kuhusisha miti inayotokana na mazao ya korosho, maparachichi na kahawa hivyo kuongeza wigo wa fursa.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo akiwa katika picha ya pamoja na wawekezaji wa hewa ya ukaa kutoka Kampuni ya Carbon Exchange Market na Relevant Co.Ltd. pamoja na wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais mara baada ya kikao cha kujadili namna ya kushirikiana katika uwekezaji huo.

Itakukumbukwa kuwa Mkutano wa 26 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi uliofanyika mjini Glasgow nchini Scotland miongoni mwa ajenda kuu ilikuwa ni namna ya nchi inaweza kufaidika na biashatra ya hewa ya ukaa.

By Jamhuri