Kila mwaka katika mwezi Februari, maelfu ya mashabiki wa muziki kutoka katika kila pembe ya dunia wanakusanyika katika eneo la Ngome Kongwe, Mji Mkongwe kuonja ladha ya kipekee ya muziki wa Kiafrika katika Tamasha la Sauti za Busara.

Tamasha hili hutoa fursa nyingi, mbalimbali ikiwemo za kibiashara katika fani tofauti pia wenye vipaji hupata fursa ya kupiga hatua za juu zaidi, na kuonekana kwa mapromota mbalimbaliambao wameudhuria hafla hiyo.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Tamasha hilo, Yusuf Mahmoud alipokuwa akiongea na waandishi wa habari.

 

“Hili siyo tu tukio ambalo watumbuizaji pekee huhudhuria, bali hata wanamuziki ambao hawapo katika orodha ya kutumbuiza huja kwa minajili ya kujifunza kutoka kwa wale wanaofanya maonesho mbalimbali, na pia hupata fursa ya kufahamiana na wadau muhimu wa tasnia yao na kutengeneza mahusiano ya kikazi kwa siku sijazo baada ya tamasha kuisha,” amesema Mahmoud.

Akaongeza “Kuelekea kuadhimisha miaka 15 toka kuanzishwa wake tamasha hili linatarajia zaidi ya wanamuziki 400 kutumbuiza ambao watatoka sehemu tofauti kama vile Afrika, Ulaya na mahali pengine, na linatoa jukwaa la kipekee kwa wanamuziki wa Afrika Mashariki kuutanganza muziki wao duniani.”

“Kila mwaka, wasani wanaopata fursa ya kutumbuiza katika jukwaa la Sauti za Busara, hualikwa katika miji mbalimbali duniani na kufanya maonesho kwenye matamasha yanayofanyika katika nchi hizo. Wanamuziki ambao hupata fursa ya kualikwa aghalabu, ni wale ambao wamethibitika katika maonesho yao kuwa wabunifu, wenye kuzungumza ujumbe fulani, na wanaocheza muziki wenye utambulisho fulani,” anasema Yusuf.

Kwa upande wa changamoto Mkurugenzi huyo akabaibisha kuwa “Changamoto kubwa inayoikumba tamasha hili ni ufadhili, na ndiyo sababu hata tamasha la mwaka 2016 lilifutwa na kusababisha hasara kubwa sana kwa biashara nyingi visiwani Zanzibar.” Akasisitiza “Tunaendelea kutegemea fedha za wahisani kutoka katika balozi mbalimbali, ambapo balozi za Norway na Uswisi zikiwa miongoni mwa wafadhili wakubwa, zikisaidia mafunzo na jitihada za ujengaji uwezo.”

Baadhi ya vikundi vya Sanaa vitakavyo pata nafasi ya kutumbuiza kwa upande wa Tanzania ni Msafiri Zawose, Jagwa Music, Leo Mkanyia, Tausi Women’s Taarab na Maulidi ya Homu ya Mtendeni

By Jamhuri