Na Mwandishi Wetu, JAMHURI MEDIA, Tanga.

Ujumbe wa Waziri wa Afya Ummy Mwalimu umewasimamisha kazi watumishi watatu kupisha uchunguzi na wengine 26 kutoka idara mbalimbali wakiendelea kufanyiwa uchunguzi kwa kukwamisha utoaji huduma kwa wananchi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga ya Bombo.

Ujumbe huo ukiongozwa na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel umefanya maamuzi hayo leo wakati akizungumza na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo wakati wa ziara yake ya siku moja kufuatilia maelekezo ya Waziri wa Afya Ummy Mwalimu juu ya kero kwa

Dkt. Mollel amesema watumishi watatu waliosimamishwa kazi ni Daktari Bingwa wa Mifupa, Mtaalam wa Usingiz na Muuguzi wa Chumba cha Upasuaji. “Tunaendelea kufanya uchunguzi katika idara zote za Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga – Bombo na watumishi wengine 26 wanaendelea kuchunguzwa zaidi,” ameeleza Dkt. Mollel.

Dkt. Molel ametoa onya kali kwa madaktari wote nchini wenye tabia za kutoa rufaa kwa wagonjwa bila sababu za msingi za matibabu kutoka kwenye Hospitali za Serikali na kuwapelekea
kwenye hospitali binafsi.

SOMA PIA;

Aidha, amesema wamiliki wa hospitali binafsi wanatakiwa kufuata taratibu na kanuni zilizopo katika kuendesha hospitali zao kwani yeyote atakayebainika kuwarubuni madaktari wa hospitali za Serikali kutoa rufaa bila sababu ya msingi ya kimatibabu watachukuliwa hatua za kisheria.


“Sio kwamba tunawakataza madaktari wa Serikali kufanya kazi baada ya muda wa serikali kuisha lakini isiwe muda wao wa kazi wanakwenda kufanya kazi kwenye hospitali binafsi na kusababisha wagonjwa kutopata huduma katika hospital za serikali,”amesema Dkt.Mollel

Dkt. Mollel ametoa rai kwa watumishi wa afya nchini kuhakikisha wanazingatia miiko na maadili ya viapo vya taaluma zao ili kuhakikisha wanaleta ubora wa huduma katika hospitali zote nchini.


Vile vile ametumia fursa hiyo kuwakumbusha watumishi wa afya nchini kuwa kipaumbele cha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ni ubora wa
huduma za afya kwa wananchi wote bila kujali hali zao za kiuchumi.

By Jamhuri