Mrembo Zari Hassan maarufu Zari The boss Lady amefunguka na kueleza kuwa hana mpango wowote wa kurudiana na mzazi mwenzake Diamond Platinumz.

Zari aliyasema hayo, alipokuwa akifanya mahojiano na shirika la Utangazaji cha Uingereza (BBC),  na kuongeza kuwa uamuzi alioufanya haukuwa wa kukurupuka na alifikiria kwa muda mrefu kabla ya kufikia uamuzi huo.

“Nilikaa muda mrefu nikafikiria vitu vingi ndipo nikasema unajua nini, nahitaji kufikia mwisho wa hili,” alisema Zari alipoulizwa kuhusu uamuzi wake wa kuachana na Diamond.

Zari aliongeza kuwa baada ya kutokea kwa skendo ya Diamond kuzaa na mtu mwingine wakiwa bado kwenye uhusiano, alijitahidi kukaa na kuyatengeneza yeye na mwenzake lakini kutokana na kuwepo kwa muendelezo wa matukio kama hayo, basi aliamua kutangaza uamuzi huo.

“Tulikuwa tunajaribu kuona tunamove kutoka scandal (kashfa) ya kuwa amepata mtoto na tunaweza kusonga mbele. Lakini vitu kama hivi leo unasikia hivi leo unaona vile sijui kukumbatiana na ma X kwenye public, vitu vya kunidhalilisha, kunifanya nisiheshimike na watoto wangu, nimeachana naye kabisa,” alisema.

Alipoulizwa kama Diamond ameshamtafuta na kuomba msamaha kuhusu vitendo hivyo, Zari alisema hakuona haja ya kufanya hivyo, kwa kuwa siyo mara ya kwanza kwani wakati yeye (Diamond) alipozaa na Hamisa aliomba msamaha lakini vitendo vyake vikaendelea kujirudia.

“Si alishakuja kipindi fulani alipozaa na huyo dada fulani (Hamisa Mabeto) sioni kama itawezekana,” alisema Zari.

Hata hivyo, alipoulizwa kama tukio la kuachana na Diamondi ni kiki ama ni ujio wa ‘project’ mpya, Zari alithibitisha kuwa ameachana nae na hakuna kingine nyuma yake.

“Yaani tumeachana kabisa, it’s done. Sijui kama amekubali, tangu video zile zimetoka na X wake nimem-block wiki tatu hatuongei ndipo nika-post,” alisema.

By Jamhuri