Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Zaidi ya shilingi bilioni 3.7 zimechangwa ikiwa ni fedha taslimu na ahadi katika hafla ya kuzichangia timu za Taifa za Tanzania ambapo kati ya hizo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amechangia shilingi milioni 500.

Fedha hizo zilipatikana kutoka kwa wadau katika sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na wizara na taasisi za Serikali, taasisi za kifedha, mashirika ya hifadhi za jamii, wafanyabiashara na wasanii pamoja na njia ya mnada ambapo jezi zenye majina ya wachezaji wa timu ya Taifa iliyoshiriki AFCON miaka ya 1980 ziliuzwa na jezi iliyouzwa na gharama kubwa ilikuwa ya golikipa Juma Pondamali iliyonunuliwa kwa shilingi milioni 25.

Rais Dkt. Samia ametoa mchango huo jana usiku Jumatano, Januari 10, 2024 wakati alipompigia simu Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa ajili ya kuzungumza na wadau mbalimbali wa michezo walijitokeza katika hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuzichangia timu za Taifa.

“Wito wangu na ombi langu kwenu Watanzania wenzangu tuchangie timu zetu ili ziende kuwakilisha vizuri jina la Tanzania. Serikali imejitahidi na imehamasisha na timu zetu zinasonga mbele, michezo ni gharama ndugu zangu. Mimi na marafiki zangu kwa kuanzia tutachangia shilingi milioni 500” amesema.

Waziri Mkuu ambaye aliongoza harambee hiyo kwa niaba ya Rais Dkt. Samia amesema lengo la kukusanya fedha hizo ni kuziwezesha timu za Taifa zinazoshiriki katika michuano mbalimbali ya kimataifa kusonga mbele. “Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi thabiti wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeshuhudia mageuzi makubwa sana katika sekta ya michezo.”

Waziri Mkuu amesema mageuzi hayo yametokana na jitihada na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali pamoja na wadau mbalimbali yakiwemo makampuni pamoja na watu binafsi, ambapo utashi mkubwa wa kisiasa katika sekta ya michezo umeleta msukumo chanya unaoongeza ari na morali kwa wadau wa sekta ya kuunga mkono na kuzienzi jitihada za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika uwekezaji na mabadiliko makubwa katika sekta ya michezo.

Amesema kwa upande wa mpira wa miguu, Timu ya Taifa ya mpira wa miguu ya wanaume “Taifa Stars” imefuzu kucheza mashindano ya AFCON yanayofanyika nchini Ivory Coast mwezi huu Januari 2024. “Ninayo furaha kuwataarifu kuwa hivi sasa timu yetu ipo kambini nchini Misri na tayari Mheshimiwa Rais amekwisha kutoa fedha za kusaidia Timu ya Taifa kushiriki mashindano haya.”

Vilevile, Waziri Mkuu amesema timu ya Taifa ya wanawake ya Mpira wa miguu “Twiga Stars” imefuzu kucheza mashindano ya WAFCON ambayo yatafanyika mwaka huu nchini Morocco, timu hiyo nayo imepewa bonasi ya Mheshimiwa Rais ya shilingi milioni 200 ilipofuzu mashindano hayo.

Awali,Mwenyekiti wa kamati ya hamasa ya kuchangia timu za Taifa, Bw. Theobaid Sabi amesema kamati yao ina majukumu makuu matatu ambapo la kwanza ni kutafuta fedha kwa ajili ya kugharamia timu za Taifa zinazotarajia kushiriki mashindano ya kimataifa, kuuelimisha umma kuhusu uwepo na umuhimu wa timu za Taifa na kuuhamasisha kuziunga mkono na kuzichangia timu hizo.

Sabi ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NBC amesema lengo ni kukusanya shilingi bilioni 10, hivyo amewaomba wadau wajitokeze kwa hali na mali kuchangia timu hizo. Amesema Benki ya NBC itaanza kuchangia shilingi milioni 100.

By Jamhuri