Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi wakati wa ziara yake ya kuimarisha uhai wa chama, kusikiliza kero za wananchi na kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020/2025, aliyoendelea nayo mkoani humo kwa kuzuru Jimbo la Mpanda Mjini.

Baada ya kutembelea na kujionea maendeleo ya ujenzi wa hospitali hiyo leo Jumamosi Oktoba 7, 2023, Komredi Chongolo ameahidi kwenda  kuweka msukumo kwa serikali kuhakikisha wanapeleka haraka sh. bil. 5 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa mradi huo wa afya pamoja na kujenga jengo la kuhifadhia maiti hospitalini hapo.

Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo, Dkt. Serafini Kisengi Patrice amesema kuwa kwa Mwaka wa Fedha 2023/24 Serikali imetenga jumla ya shilingi Bilioni 5,000,000,000 kwa ajili ya kuhakikisha ujenzi wa hospitali hiyo unakamilika kwa wakati ili wananchi wapate huduma zilizokusudiwa.

“Tunampongeza na kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa hospitali hii,” amesema Dkt. Kisengi.

By Jamhuri