Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel, amesema ameridhishwa na mabadiliko yanayofanywa na Bohari ya Dawa (MSD) hususani katika utendaji na utekelezaji wa mikataba ya upatikanaji wa dawa na vifaa tiba nchini.

Dk. Mollel amesema hayo jana mkoani Mtwara katika ziara ya kikazi akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. John Jingu walipotembelea ofisi za Bohari ya Dawa Kanda ya Mtwara, kujionea hali ya utoaji wa huduma na changamoto ya ufinyu wa ghala unaoikabili kanda hiyo.

Akizungumza na watumishi wa Kanda hiyo, Dk. Mollel amesema, ameridhishwa na mabadiliko yanayofanywa na MSD hususani katika utendaji na utekelezaji wa mikakati ya upatikanaji wa dawa na vifaa tiba nchini.

Aliongeza kuwa hatua ya Serikali kuazimia kuipatia MSD mtaji ni ya kujivunia, kwani itasaidia kuhakikisha MSD inatekeleza mipango mikakati yake, ikiwemo ujenzi wa maghala na kuhakikisha dawa na vifaa tiba vinapatikana nchini kote.

Sambaba na kutemebelea ofisi za Kanda hiyo, Uongozi huo pia ulizuru eneo la Mikindani Mkoani Mtwara, ambalo lipo mkabala na hospitali ya rufaa ya kanda ya kusini, mahali linapojengwa ghala jipya la Bohari ya Dawa Kanda ya Mtwara na kujionea jinsi mchakato wa ujenzi wa ghala hilo unavyoendelea.

Dk. Mollel ametumia fursa ya ziara hiyo, kuwapongeza watumishi wa MSD Mtwara kwa juhudi na kujituma kwao katika kuwahudumia wananchi licha ya changamoto ya udogo wa ghala uliopo.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Jingu, amewataka watumishi hao kutobweteka na kuendelea kufanya kazi kwa bidii kwani serikali inaendelea kufanyia kazi changamoto zinazowakabili, ikiwemo tatizo la ufinyu wa ghala hali inayosababisha ujenzi wa ghala jipya na la kisasa.

Ameongeza kuwa ziara yao katika Kanda hiyo, ni kudhihirisha kwamba wanatambua changamoto iliyopo, hivyo kwa kushirikiana na viongozi wengine wanaendelea kufanyia kazi changamoto hiyo, ili kupata tatuzi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, amesema taasisi hiyo kupitia mpango mkakati wake, iko katika mchakato wa maboresho ya huduma na utendaji kazi, ikiwa ni pamoja na ujezi wa maghala kwenye kanda tofauti nchini.

Amesema hatua hiyo itapanua wigo na uwezo wa MSD katika kuwahudumia wateja wake kikamilifu, kwani itaongeza uwezo wa MSD kuhifadhi bidhaa za kutosha kwaajili ya wateja na kupunguza gharama kubwa za uendeshaji.

Mavere amezitaja Kanda hizo zitakazofikiwa na maboresho ya maghala kuwa ni pamoja na Mtwara, Mwanza, Kagera na Dodoma kwa kuanzia na baadaye kuangalia kanda nyingine zenye uhitaji.

By Jamhuri