KAIMU Mkurugenzi Mkuu, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a amewasisitiza watafiti mbalimbali nchini kutumia fursa zilizopo katika Jopo hilo kwa kushiriki kikamilifu na kutoa mchango wa sayansi ya mabadiliko ya hali ya hewa ngazi ya nchi.

Dkt. Chang’a ameyasema hayo hivi karibuni wakati akizungumza na wanasayansi, watafiti, viongozi na watumishi kutoka Idara mbalimbali za Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ikiwa ni moja ya mkakati wa kuhimiza na kuongeza mchango wa nchi za Afrika kwenye ripoti mbalimbali zinazotolewa na Jopo hilo la Kimataifa.

“Huu ni mkutano wangu wa kwanza kama Makamu Mwenyekiti wa IPCC nikiwa na jukumu la kuhamasisha ushiriki wa Afrika katika mchakato na kazi za IPCC, ikiwemo maandalizi ya Ripoti ya Saba.

Viongozi wa sasa wa IPCC kutoka Afrika tumejipa jukumu la kuhamasisha na kuhakikisha ongezeko la ushiriki wa watafiti kutoka Afrika katika Jopo la IPCC. Aidha, niwajulishe kuwa mchakato wa ripoti hiyo, unatarajiwa kuanza hivi karibuni”. Alisema Dkt. Chang’a.

Naye, Mkurugenzi wa Taasisi ya Tathmini Rasilimali, UDSM Prof. Joel Kirway amempongeza Dkt. Chang’a kwa kuchaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa IPCC na kuitikia mwaliko wa kukutana na watumishi mbalimbali wa UDSM ili kuwasilisha mada ya fursa zilizopo katika Jopo la IPCC kwa Chuo cha Dar es Salaam ambacho kina Kituo cha Taaluma za Mabadiliko ya Tabianchi, kwa kutambua mchango katika maendeleo ya nchi na Afrika kwa ujumla.

Aidha, baada ya majadiliano ya kina, Prof. ameahidi kutoa ushirikiano kwa kushirikisha idadi kubwa ya watumishi na wanachuo ili kuleta mabadiliko chanya katika machapisho mbalimbali ya IPCC.

Kaimu Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a akitoa hamasa kwa watafiti mbalimbali kutumia fursa zilizopo kwenye jopo la kimataifa kupitia mkutano wa elimu ya uelewa juu ya shughuli zinazofanywa na IPCC na UNFCCC uliofanyika katika ukumbi wa IRA, UDSM jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Tathmini Rasilimali UDSM, Prof. Joel Kirway akitoa shukurani kwa Dkt. Chang’a kwa kuitikia mwaliko wa kukutana na watumishi wa UDSM ili kupata elimu ya uelewa wa Shughuli zinazofanywa na IPCC na UNFCCC kupitia mkutano uliofanyika katika ukumbi wa IRA, UDSM, jijini Dar es Salaam

Washiriki wa mkutano wakichangia mada baada ya kupata uelewa juu ya fursa zilizopo kwenye jopo la kimataifa kupitia mkutano wa elimu ya uelewa juu ya shughuli zinazofanywa na IPCC na UNFCCC uliofanyika katika ukumbi wa IRA, UDSM,  jijini Dar es Salaam
Mratibu wa Kituo cha Taaluma za Mabadiliko ya Tabianchi-UDSM, Dkt. Edmund Mabhuye akishukuru kwa kupata uelewa juu ya fursa zilizopo kwenye jopo la kimataifa kupitia mkutano wa elimu ya uelewa juu ya shughuli zinazofanywa na IPCC na UNFCCC uliofanyika katika ukumbi wa IRA, UDSM jijini Dar es Salaam

By Jamhuri