Majeneza yenye miili ya watu 19 waliofariki katika ajali ya ndege ya Precision Air iliyotokea Jumapili Novemba 6, 2022 kwa kuzama katika Ziwa Victoria, Bukoba mkoani Kagera.

Mkuu wa Mkoa wa Kagera Albert Chalamaila ametoa kiasi cha Shilingi Milioni moja kwa Kijana anayefahamika kwa jina la Majaliwa baada ya kuokoa manusura wa ajali ya Ndege ya Kampuni ya Precious Air iliyotokea mkoani Kagera ambayo ilisababisha vifo vya watu 19.

RC Chalamila, ametoa kiasi hicho cha fedha kwa Kijana huyo mbele ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati wa zoezi la kuaga miili ya waliofariki dunia kwenye ajali hiyo katika uwanja wa Kaitaba mkoani humo.

Hata hivyo, RC Chalamila ameiomba Serikali kutoa kiasi cha fedha kutoka Mfuko wa Maafa ili kufanikisha mafunzo maalum ya ukoaji kwa Wavuni wa Ziwa Victoria.

Baada ya kupewa fedha hizo (Milioni Moja) Kijana huyo Mvuvi alishindwa kujizuia na kumwaga machozi huku akipewa mkono wa pongezi na Waziri Mkuu Majaliwa kwa ushujaa wake.

Licha ya kufanikisha kuokoa baadhi ya Watu katika ajali hiyo, Kijana huyo alipoteza fahamu akidai kuwa alipigwa na kamba kichwani kwake akiwa katika harakati hiyo uokozi.

Kupitia hotuba yake, RC Chalamila amemuomba Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa kutoa taarifa zaidi kuhusu Abiria waliokwama kusafiri kwenye uwanja wa Ndege wa Kagera baada ya kutokea ajali hiyo Ziwa Victoria.

By Jamhuri