Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Arusha

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Jerry Silaa amewaelekeza wataalamu wa sekta ya ardhi nchini kuhakikisha mipango yote ya kupima viwanja inaendane na miundombinu ya maeneo husika.

Silaa ametoa maagizo hayo Oktoba 6, 2023 jijini Arusha wakati akizungumza na uongozi pamoja na watendaji wa sekta ya ardhi akiwa katika ziara yake ya siku moja mkoani Arusha.

‘’Wataalamu wote wa sekta ya ardhi nchini mnapoandaa mipango ya upimaji viwanja mhakikishe ina miundombinu itakayosaidia wananchi wanaouziwa viwanja kupunguza gharama za makazi na maisha yao’’ amesema.

Amesema ili sentesi ya jina la Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ikamilike lazima wataalamu wanapopima viwanja basi viwanja hivyo viwe na uwezo wa kusaidia huduma za miundombinu kwenye nyumba iliyojengwa pamoja na makazi.

Kwa mujibu wa Waziri Silaa, suala hilo lazima liendane na aina ya uendelezaji au ujenzi ili mhusika afahamu kama kiwanja alichochukua atajenga nyumba ya aina gani kama ni ya chini ama ghorofa.

Akielezea zaidi kuhusu zoezi la kupanga, kupima na kumilikisha (KKK) Silaa amesema, katika kipindi hiki anachohudumu wizara ya ardhi mkazo wake mkubwa utakuwa kwa zile K mbili za Kupanga na Kupima ambapo amesisitiza kuwa, maeneo yote yanayoenda kupimwa ardhi basi wataalamu wasijifungue kama wataalamu wa fani moja na kuwaachia watu vichaka.

‘’Mipango sasa ya kupanga na kupima iende ikahusishe miundombinu na kuitaja mundombinu ya barabara, maji, umeme, maji taka na mkongo wa mawasiliano ili mtu atakayekabidhiwa kiwanja kiwe mtu anaweza kuishi.

By Jamhuri