Mpango atoa pole msiba wa dada wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango leo tarehe 17 Oktoba 2022 ameshiriki ibada ya kuaga mwili wa Bi.Grace Makalla ambaye ni Dada wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Amos Makalla, Ibada iliofanyika katika Kijiji cha Kidudwe – Turiani Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro.

Makamu wa Rais amewasilisha salamu za rambirambi kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa familia ya mkuu wa mkoa wa Dar es salaam na wote walioguswa na msiba huo. Amewaasa waombolezaji kuendelea kumuombea marehemu apumzike kwa amani na kuishi yale mema aliyoyatenda enzi za uhai wake.

Aidha Makamu wa Rais amewasihi waombolezaji kuendelea kutafakari na kuishi vema katika jamii kwa kuwa msaada na neema kwa wengine hususani wenye uhitaji kama alivyoishi Bi. Grace Makalla. Amesema ni muhimu jamii kuendelea kushirikiana na kuungana wakati wa matatizo ili kuwafariji wale wanaokumbwa na changamoto mbalimbali.

Bi. Grace Makalla alifariki tarehe 14 Oktoba 2022 na amezikwa Kijiji kwao Kidudwe Turiani Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro leo tarehe 17 Oktoba 2022.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Philip Mpango akisaini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Bi. Grace Makalla ambaye ni Dada wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Amos Makalla, mara baada ya kuwasili katika msiba huo Kijiji cha Kidudwe Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro leo tarehe 17 Oktoba 2022
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Philip Mpango akiungana na viongozi , wananchi mbalimbali pamoja na  Familia ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Amos Makalla wakati wa Ibada ya kuaga mwili wa  Bi. Grace Makalla ambaye ni dada wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam mara baada ya kuwasili katika msiba huo Kijiji cha Kidudwe Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro leo tarehe 17 Oktoba 2022