1: Sioni pa kuanzia, Kueleza taarifa,

Nchi yetu Tanzania, Imekumbwa na maafa,

Taifa zima twalia, Ni msiba wa taifa,

Watu mia na zaidi, Leo tumewapoteza.

2: Raia kwa wanafunzi, Na wazazi kwa watoto,

Wametujaza simanzi, Na mili kuwa mizito,

Mili imeshika ganzi, Ni kwa hili jambo zito,

Jamani watanzania, Tuwaombee wenzetu.

3: Tumeumbiwa upofu, Kifo kwetu bado fumbo,

Ijapo tunayo hofu, Ya kifo tangu kitambo,

Tutembeapo tu wafu, Tulijue hili jambo,

Kifo hakibishi hodi, Popote waweza kufa.

4: Japo ni mengi mawazo, Vichwani yalotufika,

Kutafakari tatizo, Kwa ndugu walotutoka,

Ya nchi maombolezo, Msiba umetufika,

Jama tupige magoti, Kumrudia Muumba.

5: Leo ni wana Ukala, Imetimu yao zamu,

Tuwaombee kwa sala, Ili wafike kuzimu,

Ingawaje hili suala, Linaacha swali gumu,

Je, tatizo ni ubovu, Au chanzo ni uzembe?

6: Maswali najiuliza, Nini chanzo cha ajali?

Nani wa kunileza, Ijue yangu akili?

Tukio linaumiza, Wananchi serikali,

Ndugu wana Bugolora, Mamia tumewazika.

7: Twaomba wawajibishwe, Wote waliohusika,

Kwenye vyombo wafikishwe, Tena iwe kwa haraka,

Uzembe na ukomeshwe, Kabla hatujazika,

Tukio linaumiza, Kupoteza nguvu kazi.

8: Yapungua yangu kasi, Si kama ile ya mwanzo,

Kwa hili wingu jeusi, Vyema tutafute chanzo,

Wananchi na Rais, Ajali itupe funzo,

Haya yaliyotokea, Kesho yasijirudie.

9: Nimefikia tamati, Machungu kuelezea,

Kwenye wa tisa ubeti, Ndipo ninapokomea,

Nizionapo maiti, Kwa uchungu ninalia,

Ya mv Nyerere, Yametuachia kovu.

Mwalimu Tobias Siwingwa (Msakatonge)

                0755721609

By Jamhuri