Timu ya Simba mefanikiwa kufuzu hatua ya robo fainali katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, baada ya kufanikiwa kuichapa Horoya AC kwa mabao 7-0 katika mchezo wa Kundi C leo Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.

Mabao ya Simba SC leo yamefungwa na kiungo Mzambia, Clatous Chama matatu dakika ya 10 kwa shuti la mpira wa adhabu na 36 kwa penalti na dakika ya 70.

Mengine yamefungwa na mshambuliaji Mkongo, Jean Toria Baleke Othos mawili, dakika ya 32 na 65 na kiungo wa Mali, Sadio Kanouté mawili pia, dakika ya 54 na 87.

Mechi nyingine ya Kundi C leo, wenyeji Vipers wametoka sare ya kufungana 1-1 na Raja Casablanca Uwanja wa St. Mary’s, Kitende nchini Uganda.

Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi tisa na kupanda nafasi ya pili, nyuma ya Raja Casablanca yenye pointi 13 na wote wanafuzu Robo Fainali wakiziacha Vipers na Horoya safari yao ikiishia hapa.

Simba itamaliza na Raja Jijini Casablanca Machi 31, wakati Vipers watamenyana na Horoya Jijini Conakry nchini Guinea

By Jamhuri