Na Pamela Mollel, JamhuriMedia,Arusha

Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) William Mwakilema ametoa ufafanuzi wa tukio la vurugu zilizotokea kitongoji cha Jangwani eneo la Mto wa Mbu wilayani Monduli mkoani Arusha ambazo zimesababisha mtu mmoja kupoteza maisha na watu saba kujeruhiwa

Akizungumza kuhusu tukio hilo, leo Mei 24, 2023 Kamishina Mwakilema amesema askari wa hifadhi ya Manyara wakiwa doria ya kawaida eneo la ziwa Manyara walikamata wavuvi watatu waliokuwa wakivuwa samaki eneo lililohifadhiwa

Amesema katika tukio hilo walijitokeza wavuvi wengine na kuanzisha vurugu iliyosababisha askari hao wa uhifadhi kushindwa kuwachukuwa watuhumiwa na kwenda kutoa taarifa kituo cha Polisi

Ameongeza kwamba wakati vurugu zikiendelea umati mkubwa wa watu hao ulikwenda ofisi ya kijiji cha jangwani na kufanya uharibifu mkubwa katika ofisi hiyo ya serikali kwa kuvunja madirisha.

Pia wakachana bendera ya Taifa na kuondoka nayo kwa madai kuwa wavuvi wenzao wamezamishwa maji wakati wanakamatwa na askari wa uhifadhi

Aidha kundi hilo likiwa njiani kuelekea kuvamia ofisi na makazi ya TANAPA walifanya uharibifu mkubwa wa magari kwa kutumia marungu,mapanga na mawe kuzuia watumiaji wa barabara kuendelea na shughuli zao

“Kutokana na vurugu hizo mtu mmoja alipoteza maisha na wengine saba kujeruhiwa na kulazwa katika hospitali ya Mt.Meru wakiendelea na matibabu,hadi sasa watu 12 wanashikiliwa na jeshi la polisi kuhusiana na tukio hilo.” amesema.

By Jamhuri