Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Pwani

Mkoa wa Pwani unatarajia kuchanja zaidi ya watoto zaidi ya laki 263 chanjo ya ugonjwa wa polio katika kipindi cha kampeni hiyo ambayo itadumu kwa kipindi Cha siku nne.

Hayo yamebainishwa na Mganga mkuu wa Mkoa wa Pwani Gunini Kamba wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na kampeni hiyo ya chanjo ya polio kwa watoto wadogo.

Kamba ameongeza kuwa kampeni hiyo itawahusisha watoto wote wa Mkoa wa Pwani wenye umri chini ya miaka mitano na kwamba Maandalizi yote yanakwenda vizuri katika zoezi hilo la kampeni ya chanjo.

“Tulifanya vizuri katika awamu ya pili kwa kuvuka lengo la uchanjaji kwa asilimia zipatazo 131ya walengwa wote na hivyo tunatarajia pia kufanya vizuri katika awamu ya tatu,”amesema Mganga mkuu.

Pia Kamba amesema kwamba katika kampeni ya kipindi cha nyuma waliweza kupata ushirikiano wa kutosha kwa wananchi pindi walipokuwa wakipita katika maeneo mbali mbali ya Mkoa wa Pwani.

Mganga huyo amebainisha kwamba kampeni hiyo itaweza kusaidia kwa kiwango kikubwa kuwapatia watoto hao chanjo ambayo itaweza kuwalinda kupata maambukizi ya ugonjwa huo wa Polio.

“Kampeni hii imezinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani na kwamba kampeni hii itakuwa kwa kipindi cha siku nne na kubwa tumeshafanya hamasa na elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa chanjo kwa watoto wao,”amesema Kwamba.

Mratibu wa chanjo Mkoa wa Pwani Abasi Incha amebainisha kwamba lengo ni kuhakikisha katika kampeni hiyo ni kuwafikia watoto wote ambao ni walengwa kuwapatia chanjo hiyo.

“Tuna Imani kwamba katika kampeni hii tutapita katika maeneo mbali mbali ya Mkoa wa Pwani na kuhakikisha tunatoa matone ya chanjo dhidi ya ugonjwa wa polio katika Mkoa wa Pwani na kwamba hii itasaidia watoto kujikinga,”amesema mratibu huyo.

Pia katika hatua nyingine alitoa wito kwa wazazi na walezi Mkoa wa Pwani kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wataalamu mbali mbali wa afya ambao watakuwa wakipita katika maeneo yao lengo ikiwa ni kukamilisha zoezi hilo.
Kauli mbiu ya kampeni hiyo awamu ya tatu inasema kwamba kila tone la chanjo ya polio litaiweka Tanzania salama dhidi ya ugonjwa wa kupooza ‘polio’

Nao baadhi ya wananchi Mkoa wa Pwani wameishukuru serikali ya Mkoa huo kwa kufanya uzinduzi wa kampeni hiyo ambayo itaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kuwasaidia watoto kupata maambukizi ya ugonjwa wa Polio.

By Jamhuri