Na Dotto Kwilasa, JamhuriMedia, Dodoma

WIZARA ya Maliasili na Utalii itaendelea kutumia teknolojia katika kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu kwa kununua ndege nyuki (drones) 12 na mikanda maalum ya mawasiliano 50 (GPS Satellite Collars) kwa ajili ya ufuatiliaji wa mienendo ya wanyamapori hao.

Hayo yameelezwa leo bungeni Mei 19,2025 na Waziri wa Wizara hiyo Dk Pindi Chana wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya mwaka wa fedha 2025/2026.

Waziri Chana amesema Mikanda hiyo itafungwa kwa tembo viongozi katika maeneo yenye changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu.

Vilevile, Wizara itanunua na kusambaza mabomu baridi 40,000 katika maeneo yenye changamoto ya Tembo.

“Wizara itaendelea kufanya tafiti za kimkakati kwa ajili ya kugundua mbinu mpya za kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu.”amesema Dkt.Chana

Kamishna wa Uhifadhi Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania Musa Nassoro Kuji akiwa amesimama baada ya kutambulishwa na Mhe. Dkt. Tulia Ackson Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo Mei 19, 2025 katika Ukumbi wa Bunge jijini Dodoma alipohudhuria uwasilishwaji wa Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Katika uwasilishwaji wa bajeti hiyo Kamishna Kuji ameongozana na Makamanda wa Kanda nne pamoja na Makamishna wengine Waandamizi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA).