Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha miaka miwili madarakani imetoa zaidi ya shilingi trilioni mbili kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani Ruvuma.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Laban Thomas liyewakilishwa na Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Wakili Julius Mtatiro wakati anatoa salamu za Mkoa wa Ruvuma kwenye Ibada ya Kitaifa ya Ijumaa Kuu ambayo imefanyika katika Kanisa la Upendo wa Kristo Masihi la KIUMA wilayani Tunduru mkoani Ruvuma.

Kanali Thomas amesema kati ya fedha hizo katika kipindi cha kuanzia Machi 2021 hadi Machi 2023 kwa wilaya ya Tunduru pekee,serikali ya Rais Samia imetoa zaidi ya shilingi bilioni 223 kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani humo.

“Kati ya shilingi bilioni 223 zilizotolewa kwa Wilaya ya Tunduru pekee,shilingi bilioni 150 zinaendelea kujenga mradi msongo mkubwa wa umeme kutoka Songea hadi Tunduru,unaweza kuona Tunduru ni eneo la pembezoni hata hivyo serikali imetenga mabilioni kuhakikisha umeme wa uhakika unafika Tunduru’’;allisema RC Thomas.

Hata hivyo amesema miradi yote inatekelezwa na serikali kwa kuwa watanzania wanalipa kodi ambapo amesisitiza kulipa kodi ni wajibu wa kila mtanzania.

Kanali Thomas amewakumbusha wananchi kuweka akiba ya chakula katika kipindi hiki cha kuelekea mavuno ili familia zisipate upungufu wa chakula iwapo watauza chakula chote.

Mkuu wa Mkoa amesisitiza kuwa wakati wakristo wanaadhimisha mateso na kifo cha Yesu Kristo siku ya Ijumaa Kuu ametoa rai ,kuendelea kudumisha amani,umoja,mshikamano na utulivu wa Taifa letu.

Amesema Taifa na kanisa la Mungu litaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuwa amani na utulivu vilivyopo hapa nchini ni msingi wa kila jambo ambapo ametoa rai kwa wananchi kutoa taarifa haraka kwa mamlaka zinazohusika pale wanapoona jambo lolote linalihatarisha amani ya nchi.

Amesema wakati wakristo wanaadhimisha mateso ya Yesu Kristo,ni muhimu watanzania kuwa na upendo kwa watu wote kama alivyofanya

Yesu Kristo hivyo Kanisa la Mungu na watanzania kwa ujumla katika kipindi hiki litafakari kuhusu upendo wa kweli ambao unazaa kila kinachoonekana.

Akizungumzia kuhusu mmomonyoko wa maadili ambao unaendelea katika mataifa mbalimbali Duniani,Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma amesema mmomonyoko huo umetokana na wazazi,walezi na jamii kwa ujumla kushindwa kusimamia kikamilifu maadili ya vijana wao.

Ametahadharisha kuwa mmomonyoko wa maadili unaendelea kutishia usalama wa taifa letu ambapo amewataka wazazi na walezi kuwajibika katika malezi ya vijana wao huku akiwataka vijana kuacha kufuata utamaduni wa kishetani.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) Mkoa wa Ruvuma ambaye pia ni Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Ruvuma Mhashamu Raphael Haule akizungumza kwenye Ibada hiyo
ametoa rai kwa wazazi na walezi wa Tanzania kuwaleta Watoto wao katika misingi ya dini na maadili ya Tanzania.

Mhashamu Haule amesisitiza kuwa wazazi wakitekeleza wajibu wao vizuri Taifa la Mungu litakuwa salama ambapo ametoa rai kwa madhehebu yote kushirikiana kwa kuunganisha nguvu ili kuliokoa Taifa la Mungu na kuiponya jamii ya kitanzania hasa katika kipindi hiki cha mmomonyoko wa maadili.

By Jamhuri