Na Eleuteri Mangi, WUSM, Dodoma

Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Bw. Saidi Yakubu amekutana na kufanya kikao na baadhi ya viongozi wa Chama cha Waigizaji Tanzania (TDFAA) wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho Bw. Salum Abdul Mchoma almaarufu Chiki Choma.

Katika kikao chao viongozi hao kimefanyika Agosti 15, 2023 jijini Dodoma ambapo wamejadili masuala mbalimbali ya kuendeleza chama hicho ikiwemo maadalizi ya mkutano mkuu wa chama hicho unaotarajiwa kufanyika Septemba 2, 2023 jijini Tanga.

“Wizara ipo na ninyi, maana sekta ya maigizo hapa nchini inakua, waigizaji wana mchango mkubwa katika kuwaondolea watu msongo wa mawazo ‘stress’, watu wakimwona Mhogo Mchungu tayari wanafurahi na kutaka kumsikiliza anasema nini” amesema Katibu Mkuu Bw. Yakubu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TDFAA, Bw. Chiki Choma amesema chama hicho kina wanachama zaidi ya 56,000 katika mikoa 24 nchini na wamejipanga kuongeza wanachama wapya katika mikoa ya Rukwa na Katavi ambayo bado hawajafungua matawi.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Sanaa Bi. Leah Kihimbi, maafisa kutoka idara hiyo pamoja na Msanii mkongwe Bw. Abdalah Mkumbila almaarufu Muhogo Mchungu.

By Jamhuri